The House of Favourite Newspapers

Aliyewatikisa Zesco Atupwa nje Yanga

Balama Mapinduzi wa Yanga.

KIBOKO wa Jesse Were wa Zesco, Balama Mapinduzi wa Yanga ameondolewa kwenye orodha ya wachezaji watakaocheza na timu hiyo katika mchezo wa marudiano.

 

Yanga inatarajiwa kuvaana na Zesco katika mchezo wa marudiano wa raundi ya kwanza ya Ligi ya Mabingwa Afrika, utakaopigwa Septemba 28, huko Zambia.

 

Katika mchezo wa kwanza uliopigwa wikiendi iliyopita, Balama ndiye alionekana kikwazo kwa mshambuliaji huyo tegemeo wa Zesco baada ya kumzuia kuonyesha makali yake akianzisha mashambulizi upande wake wa kulia.

 

Akizungumza na Championi Jumatano, daktari mkuu wa timu hiyo, Edward Bavu alisema kuwa kiraka huyo anayemudu kucheza nafasi ya kiungo mshambuliaji na beki wa pembeni, alipata maumivu kwenye paja lake la kulia kwenye mchezo na Zesco.

 

Bavu, alisema kuwa kiraka huyo jana asubuhi alipelekwa hospitalini kwa ajili ya vipimo na kugundulika alipata majeraha makubwa yatakayomsababishia akae nje ya uwanja kwa muda wa wiki mbili au zaidi. Aliongeza kuwa kiraka huyo hatakuwa sehemu ya kikosi hicho kitakachorudiana na Zesco kutokana na kipindi hicho kuwepo nje ya uwanja akiendelea na matibabu.

“Balama rasmi hatakuwa sehemu ya kikosi chetu kitakachorudiana na Zesco katika mchezo wa marudiano, ni baada ya kumfanyia vipimo na kuonekana amepata maumivu makubwa kwenye paja lake.

 

“Alipata majeraha hayo tulipocheza na Zesco katika mchezo wa kwanza wa hapa nyumbani ambao alishindwa kumalizia mechi hiyo baada ya kusikia maumivu kabla ya kuomba atolewe nje.

 

“Hivyo baada ya leo (jana), kufanyiwa vipimo akaonekana amepata majeraha makubwa, atatakiwa akae nje ya uwanja kwa muda wa wiki mbili zaidi lakini nafanya jitihada za kuhakikisha anapona haraka ili arejee uwanjani,” alisema Bavu

Comments are closed.