ALIYEZAA NA GOD ZILLA AIBUKA , ANENA
DARE SALAAM SIKU chache baada ya kifo cha msanii wa Hip Hop, Golden Mbunda ‘Godzilla’ kutokea, mzazi mwenzake, Desta Minde ameibuka na kunena ya moyoni, Ijumaa Wikienda linakupa habari kamili. Akizungumza na Ijumaa Wikienda hivi karibuni, Desta ambaye amezaa mtoto mmoja na wa pekee na marehemu Godzilla, alisema enzi za uhai wa mzazi mwenzake walikuwa wakishirikiana vyema kwenye malezi ya mtoto na alikuwa akimpenda sana mwanaye.
Aliendelea kusema kuwa baada ya mzazi mwenzake huyo kufariki amekuwa akipata wakati mgumu sana kwa mwanaye kwani kila wakati anamuuliza maswali mengi kuwa baba yake yupo wapi, mara apigiwe simu ili arudi kwa sababu hajamuona wala kuzungumza naye kwa muda mrefu. “Shawn siku ile ya mazishi alikuwa ananiuliza baba yangu mbona harudi, akaenda kwa bibi yake na kumwambia ampigie simu ili arudi maana amekaa muda mrefu hajamuona baba yake.
“Tulipofika makaburini aliniuliza mbona maua haya nilikuwa najua ni ya harusi sasa hivi mmemuwekea baba, nikamwambia hapo ndipo patakuwa kwa baba na atakuwa anakaa nayo, kesho yake tulipoenda makaburini akasema anachukua maua ya baba ndipo akachukua matatu akaja nayo nyumbani, akacheza nayo akayaacha,” alisema Desta.
Aidha alisema kwa sasa anafanya utaratibu wa kumuhamishia mtoto huyo kwenye shule iliyo karibu na kwa bibi yake (mama Godzilla) anayeishi Salasala-Mbezi, Dar ili awe anamuona mara kwa mara kwani kwa sasa anasoma maeneo ya Mikocheni.
Kwa upande mwingine aliwashukuru wote ambao kwa namna moja hadi nyingine walishiriki katika kufanikisha shughuli ya kumuhifadhi katika nyumba yake ya milele. “Namshukuru Mungu kwa sababu kazi yake haina makosa kikubwa nawashukuru wote ambao walikuwa nasi katika kipindi hiki kigumu, tukishirikiana katika kila kitu hatuna cha kuwalipa zaidi Mungu awabariki sana,” alisema Desta.
Katika kuhitimisha Desta alisema ataendelea kumuenzi Godzilla kwa upendo yaani kuongeza mapenzi zaidi kwa mwanaye pamoja na familia yake kwani ni watu ambao wanampenda sana. Godzilla alifariki dunia Februari 13, mwaka huu baada ya kuugua ghafla ugonjwa wa kisukari na presha na kuzikwa katika Makaburi ya Kinondoni, Dar.
Stori: Mwandishi Wetu, Ijumaa Wikienda
Comments are closed.