BEKI wa kushoto wa Yanga, Gadiel Michael, ametangaza vita kufuatia kauli yake kwamba atajituma kuhakikisha anamshawishi kocha kumpa namba ya kudumu katika kikosi cha timu hiyo.
Michael ambaye ametokea Azam FC tangu atue katika kikosi hicho ameonekana kuaminiwa na kocha George Lwandamina ambapo kumesababisha kumweka benchi Haji Mwinyi.
Akizungumza na Championi Jumatano, Gadiel alisema kwa sasa anachoangalia katika timu yake hiyo ni kuhakikisha anajituma kwa nguvu zote ili aweze kuendelea kujihakikishia nafasi.
“Tunashukuru Mungu kuweza kufanikiwa kuibuka na ushindi dhidi ya St Louis na tumefanya vile ambavyo kocha alituelekeza na ninaamini tutafanya vyema katika mchezo unaofuata.
“Bado sijajiimarisha zaidi katika nafasi yangu hii lakini nahitaji kujituma zaidi ili niweze kuwa bora zaidi na zaidi na iwapo mwenye namba atarejea (kwenye kiwango), mwalimu ndiye aamue ampange nani lakini hakika nataka kujituma sana kila mmoja aone kazi yangu.
“Kujituma ndiyo siri ya mafanikio, naamini nitakuwa bora kwa kuhakikisha nafanya kile mwalimu anachokitaka,” alisema Gadiel.
Khadija Mngwai, Dar es Salaam
Comments are closed.