The House of Favourite Newspapers

Kafulila: Nyaraka za Tegeta Escrow Nilipewa na Mwandishi wa Habari

0
Mkuu wa Mloa wa Simiyu David Kafulila

Kwa mara kwanza tangu aibue Sakata la Akaunti ya Tegeta Escrow wakati akiwa mbunge mwaka 2014, Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, David Kafulila amesema kuwa nyaraka juu ya ufisadi huo alizipata kutoka kwa mwandishi wa habari.

 

Kafulila emesema kuwa licha ya jambo hilo kumpatia umaarufu, lakini mtu wa kwanza ambaye alitakiwa kusifiwa na kupongezwa ni mwandishi huyo wa habari ambaye alikuwa mhariri katika chombo cha habari hapa nchini (hakumtaja jina wala chombo).

 

Mkuu huyo wa Mkoa amezungumza hayo leo, Jumatano, Aprili 20, 2022 mbele za waandishi wa habari na wadau wa habari mkoani humo, katika kongamano la uhuru wa kujieleza na maadili ya uandishi wa habari lililoandaliwa na Chama cha Waandishi wa Habari mkoani humo (SMPC) kwa kushirikiana na UTPC.

 

Kafulila wakati akifungua mdahalo huo amesema kuwa nguvu ya vyombo vya habari ni kubwa sana katika kuhakikisha serikali inawajibika, hivyo vyombo vya habari vinatakiwa kujikita katika uandishi wa habari za kiuchunguzi.

 

Amesema kuwa akiwa mbunge, kupitia habari za uchunguzi na nguvu ya vyombo vya habari, aliweza kuibua ufisadi huo na kupelekea serikali kuchukua hatua kali kwa baadhi ya viongozi na wahusika.

 

“Mimi nikiwa mbunge moja ya kitu ambacho kilinipa pengine sifa kubwa nikiwa ndani ya Bunge, ilikuwa ni mapambano yangu dhidi ya vitendo vya rushwa na ufisadi hasa sakata la Escrow,” amesema Kafulila.

David Kafulila alikuwa Mbunge mwaka 2014

“Lakini Ukweli ni kwamba aliyenipa zile nyaraka za ufisadi huo ni Mwandishi wa habari ambaye alikuwa mhariri katika chombo fulani cha habari hapa nchini (hakukitaja), hapo mnaweza kuona nguvu ya vyombo vya habari ambavyo inaweza kusababisha serikali kuchukua hatua,” amesema Kafulila.

 

Amesema kuwa vyombo vya habari ni muhimu sana katika kujenga serikali inayowajibika, hivyo ni muhimu sana waandishi wa habari nchini kutambua nafasi waliyonayo katika kuiletea nchi maendeleo.

Na Derick, Simiyu

Leave A Reply