The House of Favourite Newspapers

Breaking News: Ajali ya Moto Moro, Wengine 6 Wafariki – Video

MAJERUHI wengine sita kati ya 38 wa ajali ya lori kuwaka moto ya mjini Morogoro ambao walikuwa wakitibiwa katika Hospitali ya Taifa Muhimbili, wamefariki dunia leo Agosti 14, 2019, hospitalini hapo. Idadi ya waliofariki kwa ajali hiyo sasa imefikia 82 huku majeruhi 32 wanaendelea kutibiwa.

 

Akizungumza na waandishi wa habari, Ofisa Habari wa Muhimbili, Aminiel Aligaesha, amesema majeruhi wengine 17 hali zao sio nzuri na wapo katika chumba cha uangalizi maalum (ICU) wakiendelea kupatiwa matibabu.

 

Eligaesha ametoa wito kwa wananchi wote kuendelea kuwaombea majeruhi waliobaki huku pia akiwataka kufika Muhimbili kwa ajili ya kuwachangia damu kwani idadi ya majeruhi na kiasi cha damu kilichopo bado hakitoshi.

 

Majeruhi hao walifikishwa hospitalini hapo siku nne zilizopita wakitokea mkoani Morogoro eneo ambalo ilitokea ajali ya moto uliosababishwa na lori la mafuta kulipuka na kugharimu maisha ya watu zaidi ya 70, na majeruhi ambao wapo hospitali ya mkoa wa Morogoro na wengine wapo Muhimbili.

Comments are closed.