The House of Favourite Newspapers

Chadema Yasusa Uchaguzi Muhambwe, Kigoma

0

CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), kimetangaza kutoshiriki uchaguzi mdogo katika Jimbo la Muhambwe mkoani Kigoma, kwa madai hautakuwa huru na haki.

 

Chama hicho kimetoa sababu kwamba, dosari zilizojitokeza katika Uchaguzi Mkuu 2020, hazijapatiwa ufumbuzi.
Uamuzi huo umetangazwa tarehe 1 Aprili 2021 jijini Dar es Salaam na Naibu Katibu Mkuu wa Chadema Bara, Benson Kigaila, wakati anatoa maamuzi ya Kamati Kuu ya chama hicho, kuhusu uchaguzi mdogo wa Muhambwe, uliotangazwa na Tume ya Taifa ya Uchaguzi nchini (NEC).

 

 

Kigaila ametaja dosari zilizojitokeza katika uchaguzi mkuu wa mwaka jana kuwa ni, baadhi ya wagombea wa vyama vya upinzani kuenguliwa na wengine kunyimwa fomu za kuomba uteuzi za NEC, mawakala kuzuiwa kuingia katika vituo vya kupigia kura.

 

 

“Tume hiyo muundo wake haujabadilika na watu hawajabadilika. Kama muundo haujabadilika, sheria hazijabadilika, kanuni hazijabadilika ni zile zile unakwenda katika uchaguzi kutegemea nini? Angalau wangebadilika watu tu,” amesema Kigaila.

 

 

NEC ilitangaza uchaguzi huo mdogo kufuatia kifo cha aliyekuwa mbunge wake kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), Atashasta Nditiye, kilichotokea tarehe 12 Februari 2021.

 

Kwa mujibu wa ratiba ya NEC, fomu za uteuzi zitatolewa kuanzia tarehe 28 Machi hadi 3 Aprili mwaka huu, siku ambayo pia uteuzi wa wagombea utafanyika.

 

 

Kampeni za uchaguzi huo zitafanyika kuanzia tarehe 4 Aprili hadi 1 Mei, 2021, huku uchaguzi utafanyika tarehe 2 Mei mwaka huu.

 

 

Kuhusu kushiriki uchaguzi wa Jimbo la Buhigwe, lililotangazwa kuwa wazi tarehe 30 Machi 2021 na Spika wa Bunge, Job Ndugai, baada ya aliyekuwa mbunge wake, Dk. Phillip Mpango, kuteuliwa kuwa Makamu wa Rais.

 

 

Kigaila amesema kama mazingira ya uchaguzi yataboreshwa, Chadema itashiriki uchaguzi huo. “Kwenye suala la Buhigwe ni kwamba uchaguzi ambao umetangazwa kwenye mazingira ya leo ni Muhambwe, tunazungumza Muhambwe kwa sababu ya mazingira haya ya leo ambayo hayajabadilika.

 

 

Tunajua madhila ya mwaka jana na madonda ya mwaka jana hayajapona, Buhigwe kama mazingira yatabadilika tutashiriki,” amesema Kigaila.

 

 

Katika Uchaguzi Mkuu wa 2020, vyama vya upinzani viliambulia majimbo sita kati ya majimbo zaidi ya 360, huku Chadema kikiambulia jimbo moja la Nkasi Kaskazini.

Leave A Reply