The House of Favourite Newspapers

Compact Energies Yashinda Tunzo Ya Mwaka

0
Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Compact Energies, Ephraim Kimati (mwenye miwani) akipokea zawadi ya Kampuni Bora ya uzalishaji wa umeme wa jua nchini Tanzania (Solar Energy Company of the Year) kutoka kwa Tike Mwakitwange, Ofisa wa MultiChoice kwenye Tuzo za Kampuni Bora Afrika zilizofanyika Mlimani City Dar, Alhamisi usiku. Wengine ni Brown Mamiro, Ofisa Lojistiki wa kampuni ya hiyo na kulia ni Ofisa Masoko wa kampuni hiyo, Hassan Mseja .

Kampuni ya usambazaji na ufungaji wa vifaa vya umeme jua nchini, Compact Energies imeshinda tuzo ya ’First Runner Up- Solar Energy Company of the Year’ katika tuzo  za Africa Company of the Year Award (ACOYA) zilizoandaliwa na Eastern Star  Consulting Group katika ukumbi wa Mlimani City jijini Dar es Salaam.

Akizungumza mara baada ya kupewa tuzo hiyo katika utoaji wa huduma bora ya nishati ya umeme jua (Solar Energy) nchini Tanzania, Mkurugenzi Mtendaji wa Compact Energies Ephraim Kimati amesema kampuni yake imekuwa mstari wa mbele katika kuleta mageuzi ya nishati mbadala katika maeneo mbalimbali hapa nchini yakiwemo maeneo ya mijini na vijijini na ndio maana imeshinda tuzo hiyo muhimu.

Amesema Watanzania wengi wanaogopoa kutumia mfumo wa umeme jua wakihofia gharama, lakini faida zake ni nyingi, ikiwemo uhakika wa kupata umeme muda wote, tena bila kulipa gharama za matumizi ya kila mwezi.

“Gharama za mwanzo za kupata umeme jua zinaweza kuwa ni kubwa, lakini baada ya hapo matumizi huwa ni ya zaidi miaka 20 au 30  bila gharama nyingine zozote,”amesema.

Amewahimiza  Watanzania kutumia nishati ya umeme jua majumbani mwao, ofisini na viwandani  ili kuwa na uhakika wa kutumia nishati hiyo ambayo gharama yake ni ndogo na hudumu kwa muda mrefu.

“Niwahimize Watanzania kutumia mfumo wa umeme jua kwa sababu sio gharama, ila unasaidia kuokoa gharama,”amesema.

Amesema mwelekeo wa dunia kwa sasa ni kutumia mfumo wa umeme jua na gesi na nchi nyingi barani Ulaya, Afrika zikiwemo zile za G7 zinasisitiza matumizi ya nishati hiyo ili kuleta maendeleo ya haraka hasa katika maeneo ya vijijini.

“Dunia sasa hivi inabadilika kuelekea nishati mbadala na ndio maana vitu vingi vinavyotengezwa hivi sasa vinatumia nishati mbadala,” amesema.

Ametoa wito kwa Watanzania kununua huduma zinazotolewa na makampuni ya nyumbani ili kukuza soko kwa maendeleo ya nchi na kukuza nguvu ya uchumi kwa nchi za Afrika ili kushindana katika soko la dunia.

Amesema wakiwa kampuni ya wazawa, wamefanya kazi kwa ufanisi katika miradi mbalimbali ukiwemo wa bomba la mafuta ghafi la Afrika ya Mashariki (EACOP) ambapo wao ndio walifunga mfumo mzima wa nishati ya jua katika nyumba walizopewa watu fidia na mradi huo mkubwa.

“Tumepata mrejesho mkubwa sana kutoka kwa watu tuliowahudumia na hata wakati tulipowakabidhi mfumo wa sola walifurahia sana.

“Tuna vifaa vya kisasa na wafanyakazi wenye weredi na kujitoa ili kuwapa Watanzania huduma bora, zenye unafuu na uhakika.”

“ Kiukweli tunaona mchango wetu mkubwa katika jamii ya Watanzania kwa kuwapa huduma ya nishati watu ambao walikuwa hawana uhakika wa umeme na hata wale ambao wamefunga kwa ajili ya kuhakikisha hawapati changamoto hata umeme ukikatia,” amesema.

Mkurugenzi wa tuzo hizo zilizoandaliwa na zilizoandaliwa na Estern Star Consulting Group,Deogratius John amesema lengo la kuanzisha tuzo hizo ni kutambua ushindani wa kibiashara wa Afrika kwa makampuni ya Afrika ili yapate utambulisho katika soko la dunia.

Amesema ushindi wa tuzo hizi zinayafanya makampuni kuaminika katika soka na kuonyesha uwezo wao katika kutoa huduma.

Amesema ana imani makampuni ya Tanzania na Afrika kwa ujumla yana uwezo wa kushindana na makampuni ya nje yaliyowekeza katika teknoloji, licha ya biashara inayofanyika ndani ya Afrika ni ndogo, ukilinganisha na biashara ambayo Marekani au China inafanya na nchi za Afrika.

Tuzo hizo zilitolewa katika Ukumbi wa Mlimani City Hall Jijini Dar es Salaam zilizohusisha makampuni na mashirika kwenye vipengele zaidi ya 80 ambapo ASA Microfinance ndio walikuwa vinara wa tuzo hizo.

Leave A Reply