Diwani Pemba Mnazi Aahidi Kuwarejeshea Wananchi Wake Ardhi Yao
DIWANI wa Kata ya Pemba Mnazi, Wilaya ya Kigamboni Dar, Lyoba Ramadhani Yamringa, amewaondoa hofu wakazi wa kijiji cha Tundwi Songani na Pemba Mnazi ambao hati za awali za umiliki viwanja vyao (vocha) 52, zinashikiliwa na mwanasheria wa mwekezaji waliyetaka kumuuzia ardhi yao lakini wakashindwana.
Wanakijiji hao walishindwana biashara na mwekezaji huyo wakati hati zao walishampa mwanasheria wake ambaye anaendelea kuzishikiliwa kwakuwa anawadai pesa aliyowakopesha kwa ajili ya kuzifuatilia hati hizo serikalini.
Kufuatia hati hizo kushikiliwa na mwanasheria huyo wananchi hao kilio chao kikubwa ni kushindwa kumuuzia mtu mwingine kuliendeleza eneo hilo kwakuwa hawana hati hizo mikononi mwao.
Baada ya kilio cha miaka kadhaa cha wanakijiji hao ndipo diwani Lyoba alianza kufuatilia suala hilo na kufikia hatua ya kukubaliana na mwanasheria huyo kuwarejeshea hati zao na kumlipa pesa anayowadai kwa utaratibu utakaopangwa na serikali ya kijiji hicho.
Diwani Lyoba aliwaahidi wananchi hao neema hiyo kwenye mkutano na wanakijiji uliofanyika ofisi ya Serikali ya Kijiji cha Songani.
Diwani Lyoba aliwaahidi wanakijiji hao kuwarejeshea hati zao hizo Julai 23 mwaka huu kauli ilizusha shangwe na nderemo kwa wanakijiji hao ambao wengine walishakata tamaa na ardhi yao na kuhisi huenda walishanyang’anywa.
Akizungumza kwenye mkutano huo uliojaa furaha na nderemo kwa diwani huyo alisema;
“Mama zangu na baba zangu kwenye kata yangu mimi kama diwani wenu hakuna mtu atakayenyang’anywa ardhi yake kiuonevu mimi nikiwepo, najua nyinyi ndiyo waanzilishi wa maeneo haya ndiyo maana mmemilikishwa na serikali.
Ni kweli mlitaka kumuuzia mwekezaji sehemu ya ardhi yenu sasa mliposhindwana biashara mkajikuta hati zenu ziko mikononi mwake na kuwafanya mshindwe kufanyabiashara na mtu mwingine au kuyaendeleza kwakuwa hati zenu zimeshikiliwa na mtu mwingine.
“Hivyo nimwaambie tena kuwa hizo hati nimeshazipambania na nitazirejesha hapa ofisi ya kijiji Julai 23 mwaka huu na utaratibu wa kila mtu kupewa hati yake utafanyika hapa”.
Alisema diwani huyo huku akishangiliwa na wanakijiji hao ambao hati zao zinashikiliwa na mwanasheria huyo.
HABARI/PICHA: RICHARD BUKOS /GPL