WAZIRI wa Fedha na Mipango, Dkt. Phillip Mpango amesema kuwa anafurahishwa na huduma za kifedha hasa za mabenki zinapowafuata wananchi nje ya miji na kupata huduma mbalimbali bila kuhangaika kufika mjini.
Hayo ameyasema leo wakati akifungua Tawi la Benki ya ABC lililopo Tegeta nje kidogo ya Jiji la Dar es Salaam.
Akizungumza katika hafla hiyo alisema kuwa : “Namshukuru Mwenyekiti wa Bodi, Wajumbe wa Bodi, Uongozi wa Benki ya ABC kwa kunialika kufungua tawi hili la Tegeta. Mimi kama waziri wa fedha napata faraja ninapoona huduma za fedha zinakua na hasa zinapowafuata wananchi walio nje ya miji.”
Alielezea kuwa anaushukuru uongozi wote wa benki hiyo kwa kupanua huduma hiyo ili kuwafikia wananchi wengi zaidi hadi kuwafikia wananchi walio wengi vijijini.
“Serikali ingependa kuona huduma za taasisi za fedha zikielekezwa zaidi kwenye vijiji vya wilaya pembezoni ambako kuna Watanzania wengi ambao nao wanahitaji kupatiwa huduma za kibenki.”
Aidha aliwaomba uongozi mzima wa Benki ya ABC kufikisha zaidi huduma yao pembezoni mwa miji na kupata huduma za kibenki bila vikwazo na masharti magumu.
“Ni matarajio ya wengi kuwa kufunguliwa kwa tawi hili hapa Tegeta kutakata kiu ya wajasiriamali waliokuwa wakisubiri kwa hamu kupata mikopo kwani itawasaidia kuinua hali zao za maisha na pia kuchangia pato la taifa kwa kushirikiana katika uzalishaji mali kutokana na shughuli mbalimbali wanazofanya.
Naye Mkurugenzi wa Wateja Binafsi, Wafanyabiashara Wadogo na Kati, Joyce Molai aliwaomba wananchi kujitokeza katika Benki ya ABC hasa Tawi la Tegeta ili kuweza kujionea huduma wanazozitoa na kufungua akaunti za kutunza amana zao, na wateja wao kupata fursa ya kuomba mikopo nafuu ya kuendeleza biashara na shughuli nyingine za kiuchumi.
Na Denis Mtima/GPL
Comments are closed.