The House of Favourite Newspapers

Flora Mvungi Atiwa Mbaroni

 

Muigizaji Flora Mvungi.

Majanga ya Krismasi! Ndivyo unavyoweza kusema kufuatia muigizaji Flora Mvungi kujikuta mikononi mwa polisi alipokuwa akisherehekea sikukuu hiyo. Mrembo huyo alipata majanga hayo akiwa na wenzake wakipata ‘masanga’ kwenye baa moja iliyopo jirani na Kituo cha Polisi cha Urafiki na ndipo askari waliokuwa doria walipowakamata na kuondoka nao hadi kituoni hapo.

 

Awali, askari mmoja alifika katika baa hiyo na kuchimba mkwara mzito, akimtaka DJ kuzima muziki na kisha kufunga baa kwani haikuwa haki kwenda kukamata wauzaji wa baa zingine waliopitisha muda unaotakiwa kisheria (saa 5 usiku) na kuwaacha waliokuwa jirani na kituo hicho cha polisi. Hata hivyo, alipoondoka alirejea tena ndani ya dakika tano na kubaini uwepo wa Flora akiwa na jamaa mmoja aliyedaiwa kuwa ni mchepuko wake sanjari na jamaa wengine wawili.

 

“Haiwezekani sisi tunaenda kukamata wauzaji wa baa zingine huko na kuwaacha ninyi ambao mko karibu hapa, nyie askari hebu njooni haraka muwaweke ndani hawa watu maana hii sasa ni dharau,” alisikika askari huyo ambaye alionekana kuwa mkubwa kwa cheo chake.

 

Mwanahabari wetu aliyekuwa jirani na eneo hilo, alishuhudia msanii huyo na wenzake hao wakiingizwa kwenye chumba maalum cha mahojiano katika kituo hicho cha polisi. Shushushu wetu alijaribu kujisogeza kituoni hapo na kushuhudia Flora na wenzake hao wakihojiwa, huku mmoja wa askari akishangazwa na uwepo wa Flora eneo hilo kwa majira ya usiku mwingi kiasi hicho.

 

Hadi mwanahabari wetu anaondoka kituoni hapo usiku mnene, Flora aliyekuwa na wenzake walikuwa angali wanashikiliwa na polisi. Kesho yake (Jumanne) mwanahabari wetu alijaribu kumtafuta Flora kupitia simu yake ya mkononi ambapo alipokea na kukiri kutiwa mbaroni.

 

“Ni kweli tulikamatwa na marafiki zangu lakini hilo swala tulilimaliza usiku uleule tukaachiwa, si unajua tena mambo ya kuzidisha muda wao ule wa saa tano,” alisema Flora. Alipoulizwa kuhusu madai ya kwamba mmoja kati ya wanaume aliokuwa nao ni mchepuko wake, Flora alikanusha vikali.

 

“Wote ni washkaji zangu tu na tulikuwa pamoja kama kampani lakini watu huwa wanazusha kwamba ni mtu wangu jambo ambalo siyo kweli,” alisema Flora. Flora na mumewe, staa wa Bongo Fleva, Hamis Ramadhan ‘H. Baba’ kwa muda mrefu sasa wamedaiwa kutengana, japo wenyewe kwa nyakati tofauti wamekuwa wakikanusha madai hayo.

Stori: Brighton Masalu, Amani

Comments are closed.