The House of Favourite Newspapers

Funga Mdomo, Molinga Ameanza Kazi Yake Rasmi

David Molinga

MASHABIKI wa Yanga wanasema kwamba, “Funga mdomo, David Molinga ameanza kazi yake rasmi.” Kauli hiyo ya mashabiki lialia wa Yanga imekuja baada ya jana Alhamisi, mshambuliaji huyo wa kimataifa kutoka DR Congo, kuanza cheche zake za kucheka na nyavu kutokana na kufunga mabao mawili safi dhidi ya Polisi Tanzania.

 

Molinga aliyejiunga na Yanga msimu huu akitokea FC Renaissance du Congo ya DR Congo, alifunga mabao hayo katika sare ya mabao 3-3, ukiwa ni mchezo wa Ligi Kuu Bara uliochezwa kwenye Uwanja wa Uhuru jijini Dar es Salaam.

Mshambuliaji huyo ambaye wakati anawasili Yanga alikuwa na uzito wa kilo 92 uliomfanya awe mzito kuonyesha makeke, kocha wake, Mwinyi Zahera alimpa program maalum ya kupunguza uzito huo ambapo anatakiwa awe na kilo 78 na tayari uzito wake umeshaanza kupungua.

 

Mabao hayo aliyafunga dakika ya 65 kwa kichwa na 68 akipiga faulo ya kiufundi na kujaa wavuni moja kwa moja. Bao la kwanza la Yanga lilifungwa na Mrisho Ngassa dakika ya 6.

 

Wakati Molinga akifunga mabao mawili, mshambuliaji wa Polisi Tanzania, Ditram Nchimbi aliifungia timu yake mabao matatu dakika ya 34, 55 na 58.

 

Kabla ya kufunga mabao mawili jana, Zahera aliwahi kutoa ahadi kwamba anamtabiria Molinga msimu huu atafunga mabao kuanzia 15 hadi 20, huku akisisitiza kwamba, kama mshambuliaji huyo hataweza kufikisha mabao hayo, basi akatwe mkono. Ikiwa huu ni mchezo wa pili kwa Yanga msimu huu kwenye Ligi Kuu Bara, Molinga tayari amefunga mabao mawili ikiwa ni idadi kubwa ndani ya kikosi hicho.

 

Licha ya kusajiliwa washambuliaji wengi ndani ya kikosi hicho tangu kuondoka kwa Heritier Makambo, lakini inaonekana Molinga ndiye anategemewa zaidi katika kuiongoza safu hiyo ya ushambuliaji. Katika mchezo wa kwanza wa ligi kuu msimu huu, Molinga alicheza dakika zote tisini wakati Yanga ikifungwa bao 1-0 na Ruvu Shooting.

 

Katika mchezo huo wa jana, ulionekana kuwa na ushindani mkubwa huku Yanga ikiikosa huduma ya kocha wao mkuu, Mwinyi Zahera ambaye ameanza kutumikia adhabu ya kukosa mechi tatu, adhabu aliyopewa na Shirikisho la Soka Tanzania (TFF).

 

Polisi Tanzania inayonolewa na Selemani Matola, ilimaliza mchezo huo ikiwa pungufu baada ya Yassin Mustapha kutolewa uwanjani kwa kadi nyekundu.

HARMONIZE atajwa tuzo ulaya, msanii pekee kutoka Afrika Mashariki

Comments are closed.