The House of Favourite Newspapers

Yanga Kuanza Kazi leo dhidi ya Coastal Union Uwanja wa Uhuru

SARE ya mabao 3-3 dhidi ya Polisi Tanzania kwenye Uwanja wa Uhuru imewazindua Yanga. Kamati mbili nzito ndani ya klabu hiyo ile ya ufundi na nyingine ya mashindano zimekutana na wachezaji na kocha kutaka kujua kuna ishu gani na wakaweka mambo sawa.

 

Kikao cha kwanza kilifanyika Uwanjani baada ya ile sare na kingine kikafanyika klabuni ili kuhakikisha mambo yanakaa sawa na wachezaji wanacheza soka la maana kupunguza presha na minong’ono ya mashabiki kwamba baadhi ya mastaa wanazingua.

Habari za ndani ambazo Spoti Xtra imejiridhisha nazo ni kwamba Kamati ya Ufundi chini ya Boniface Mkwasa na wajumbe wake akiwemo Sunday Manara, wamelazimika kumuweka chini Zahera ili kumueleza msimamo wao na kuzidi kumtia moyo.

 

Habari zinasema kwamba kamati hizo ziliwasisitiza wachezaji kuongeza bidii ya kupambana pamoja na kucheza soka la kuvutia ili mashabiki wasikate tamaa ya kuja viwanjani. Lakini vilevile ikawasisitiza kutokata tamaa hususani wale wapya waliojiunga na klabu msimu huu kwani mapambano ndio kwanza yameanza.

Kwenye kikao hicho, Zahera kwa niaba ya wachezaji alikiri kwamba ni hali ya mchezo lakini watapambana na kutakuwa na mabadiliko makubwa kuanzia kwenye mechi ya leo dhidi ya Coastal Union kwenye Uwanja wa Uhuru. Wachezaji nao akiwemo Pappy Tshishimbi na Juma Balinya wakaahidi kupambana kiume huku uongozi ukimhakikishia Zahera kwamba kibarua chake na wachezaji wake viko salama.

 

Ingawa Makamu Mwenyekiti wa Yanga, Fredrick Mwakalebela hakuwa tayari kufafanua ishu hiyo lakini Ofisa Habari wa klabu, Hassan Bumbuli alikiri kwamba kulikuwa na vikao vya kamati hizo ili kuweka mambo sawa na kupandisha morali ya mechi ya leo.

 

MECHI YA LEO Yanga imetamba kwamba leo Coastal Union wanaumbuka Jijini Dar es Salaam. Katika michezo ambayo Yanga imecheza imeshindwa kutamba mbele ya Ruvu Shooting na Polisi Tanzania na ina alama moja tu. Akizungumza na Spoti Xtra, Mratibu wa Yanga, Hafidhi Saleh alisema; “Tunahitaji kushinda kila mchezo uliopo mbele yetu hatuna huruma kwa kila ambaye tutacheza naye malengo ni pointi tatu.

 

Lakini Sadnye Ukirhob na Lamine Moro ni majeruhi na hawatakuwa sehemu ya mchezo wa Coastal,.” Kwa upande wa kocha wa Coastal Union Juma Mgunda alisema kuwa :“Utakuwa ni mchezo mgumu ambao unahitaji umakini na kila mmoja anapambana kuhitaji ushindi hivyo kilichobaki ni kupambana.”

 

Coastal tayari imecheza mechi tatu na kuvuna alama 4. Hata hivyo kwa miaka ya karibuni Yanga imetoa sare mara moja, huku ikishinda mechi zake tatu kwenye uwanja huo.

 

Balama Mapinduzi ameliambia Spoti Xtra kuwa; “Hatutakubali kufanya vibaya katika mchezo wetu huo,tutahakikisha tunapata ushindi wetu wa kwanza ili tujiweke katika nafasi nzuri zaidi.” Pia beki Ally Mtoni alisema kuwa kufanya vibaya katika michezo miwili iliyopita kunawapa hasira na leo lazima kieleweke.

STORI NA MUSA MATEJA

JPM Amuweka MTU KATI Waziri MBARAWA Mbele Ya WANANCHI “Njoo Ueleze”

Comments are closed.