The House of Favourite Newspapers

Hakimu Atishia Kuifuta Kesi ya Mkurugenzi wa Jamii Media

Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu imetishia kuifuta kesi inayomkabili Mkurugenzi Mtendaji wa mtandao wa JamiiForums, Maxence Mubyazi Melo na mwanahisa wa kampuni ya Jamii Media Co Ltd, Mike William ikisema haifurahishwi na mwenendo wa shauri hilo. 
Hakimu mkazi mkuu wa mahakama hiyo, Thomas Simba alisema hayo jana mara baada ya Wakili wa Serikali, Hamis Said kueleza kuwa wakili anayeendesha kesi hiyo ni mgonjwa na kwamba jana ilikuwa siku ya washtakiwa kusomewa maelezo ya awali.
“Haya mambo ya kuahirishaa- hirisha kesi siyafurahii. Wakati mwingine (kama) kesi haiendelei, nafuta,” alisema Hakimu Simba baada ya wakili huyo wa Serikali kuomba kesi hiyo iahirishwe hadi Machi 20.
Hakimu Simba aliiahirisha kesi hiyo hadi Aprili 3, siku ambayo washtakiwa hao watasomewa maelezo ya awali katika kesi hiyo ambayo washtakiwa wanadaiwa kuzuia uchunguzi wa Jeshi la Polisi.
Washtakiwa hao wanaotetewa na mawakili, Tundu Lissu, Jeremiah Mtobesya, Tika Hamis, Hassan Kihangio, Fedrick Kihwelo na Masoud George, watasomewa maelezo hayo ya awali baada ya upande wa mashtaka kukamilisha upelelezi wa kesi hiyo.
Katika kesi hiyo, namba 456/2017, inadaiwa kuwa kati ya Aprili Mosi na Desemba 13 mwaka jana, wakiwa Mikocheni, wakiwa wakurugenzi wa Jamii Media ambayo inaendesha tovuti ya Jamiiforums walishindwa kutoa taarifa kwa Jeshi la Polisi ambalo lilikuwa likichunguza mawasiliano ya kimtandao yaliyochapishwa katika tovuti yao. Washtakiwa hao wapo nje kwa dhamana.

Comments are closed.