The House of Favourite Newspapers

Hali ya Bocco Baada ya Kuumia Jana Kwenye Mechi na Mwadui

 

KLABU ya soka ya Simba SC kupitia kwa msemaji wake Haji Manara imetoa taarifa kuhusu maendeleo ya mshambuliaji wake John Bocco ambaye aliumia jana kwenye mechi ya Ligi Kuu dhidi ya Mwadui FC katika Uwanja wa Kambarage Shinyanga.

 

Taarifa ya Manara imeeleza kuwa nyota huyo ambaye amesajiliwa kutoka Azam FC msimu huu anaendelea vizuri na huenda akarejea uwanjani hivi karibuni kuendelea kuitumikia klabu hiyo. 

 

”Niwajuze hali ya Bocco inaendelea vema kwa sasa na jopo la madaktari linahangaika nae ili aweze kucheza tena haraka iwezekanavyo”, amesema Manara.

 

John Bocco aliumia kipindi cha kwanza ambapo tayari alikuwa ameifungia Simba bao la kuongoza dakika ya tisa, baada ya kushindwa kuendelea nafasi yake ilichukuliwa na mshambuliaji Laudit Mavugo.

 

Mechi hiyo iliisha kwa sare ya 2-2 ambapo bao la pili la Simba lilifungwa na Emmanuel Okwi huku ya Mwadui yakifungwa na David Luhende pamoja na Paul Nonga. Bocco sasa ana mabao 10 kwenye orodha ya wafungaji msimu huu.

Comments are closed.