The House of Favourite Newspapers

HAWA NDIYO MAWAZIRI 10 WA JPM WACHAPAKAZI

KUPITIA magazeti yanayochapishwa na Kampuni ya Global Publishers na Mtandao wa Global Publishers, Kampuni ya Global Publishers LTD iliamua kufanya utafiti kutoka kwa wa­somaji kutaka kujua ni mawaziri gani wa serikali ya Rais Dk. John Pombe Magufuli, wanaoongoza kwa kuchapa kazi.

Wasomaji walitakiwa kutuma majina ya mawaziri wanaoona wanachapa kazi kwenda kwenye namba maalum iliyowekwa kwenye magazeti na hatimaye, wasomaji wengi wametoa maoni yao kuhusu mawaziri kumi wachapakazi.

Kwa kuzingatia kura zilizokuwa zikipigwa na wasomaji wetu, wafuatao ni mawaziri kumi waliopata kura nyingi zaidi, hivyo kuki­dhi kuingia kwenye orodha ya mawaziri kumi wachapa­kazi.

  1. WAZIRI MKUU, KAS­SIM MAJALIWA

Waziri Mkuu, amepigiwa kura na wasomaji wengi, wak­ieleza kwamba amekuwa mstari wa mbele kuwasimamia mawaziri pamoja na kumsaidia mheshimiwa rais katika majukumu mbalimbali. Muda mwingi anafanya ziara kwenye maeneo mbalimbali nchini, kushughulikia changamoto zinazow­akabili wananchi.

  1. WILLIAM LUKUVI

Waziri wa Nyumba na Maendeleo ya Makazi, William Lukuvi, amepigiwa kura na wasomaji wengi, wakimpongeza kwa jinsi anavyoshughulikia mi­gogoro sugu ya ardhi ambayo kwa kipindi kirefu ilikuwa ikiwatesa wananchi. Pia kutafuta suluhu ya migogoro baina ya wafugaji na wakulima, inayohusu ardhi.

  1. PROFESA MAKAME MBARAWA

Profesa Makame Mbarawa am­baye awali alikuwa Waziri wa Ujen­zi, Uchukuzi na Mawasiliano kabla ya kuhamishiwa Wizara ya Maji na Umwagiliaji, naye amepigiwa kura nyingi kutokana na uwajibikaji mkubwa aliouonesha akiwa katika wizara yake ya awali.

Akiwa Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Waziri Mbarawa alikuwa akiongoza kwa kutokaa ofisini, muda mwingi alikuwa akitembelea na kukagua miradi mbalimbali iliyopo chini ya wizara yake, kama ujenzi wa bara­bara na miundombinu mingine. Ari hiyo ameendelea nayo hata baada ya kubadilishiwa wizara na kupelekwa Wizara ya Maji na Umwagiliaji.

  1. UMMY MWALIMU

Waziri wa Afya, Maendeleo ya jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu naye anaingia katika orodha hii kutokana na kura nyingi alizopigiwa.

Wasomaji wengi wameonesha kuridhishwa na utendaji kazi wake, hasa katika kushughulikia matatizo yanayowakabili wa­nawake na watoto, upatikanaji wa huduma za afya, madawa na vifaa tiba mpaka vijijini sambamba na ubora wa huduma zinazotolewa na hospitali zetu, ikiwemo Hospi­tali ya Taifa ya Muhimbili.

  1. SELEMAN JAFO

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, Seleman Jafo pia amep­igiwa kura, wengi wakionesha kuridhishwa na namna anavyow­asimamia watendaji mbalimbali wa serikali, kuanzia ngazi ya chini kabisa, anavyoshughulikia kero za wananchi hasa zinazowahusu wa­tendaji wabovu wa serikali na jinsi anavyotembelea maeneo mbalim­bali ya nchi kutatua changamoto zinazowakabili wananchi.

  1. DKT. HAMIS KIGWAN­GALLA

Waziri wa Maliasili na Utalii, Dkt. Hamisi Kigwangalla, naye amepigiwa kura zilizomuweze­sha kuingia kwenye orodha ya mawaziri kumi wachapakazi, ambapo sifa yake kubwa ni kuto­bweteka ofisini, badala yake mara kwa mara amekuwa akitembelea kwenye maeneo mbalimbali nchini, kufuatilia jinsi maliasili na vivutio vya utalii, vinavyotunzwa na kuendelezwa.

Pia amekuwa mstari wa mbele katika vita dhidi ya ujangili, akiku­tana na maafisa wanyamapori mara kwa mara kujadiliana nao kuhusu changamoto zinazow­akabili na namna ya kuzitatua. Hivi karibuni alipata ajali mbaya ya gari, akiwa anatoka kwenye ziara ya kikazi mkoani Arusha, huu ukiwa ni uthibitisho wa namna anavyochapa kazi.

  1. HARRISON MWAKYEMBE

Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dkt. Harrison Mwakyembe naye ameingia kwenye orodha hii, akitajwa kuwa mstari wa mbele kutatua changa­moto mbalimbali zinazoikabili wiz­ara yake, kuanzia kwenye masuala ya habari, sanaa na wasanii mpaka kwenye michezo.

Changamoto iliyotajwa na wengi, ni kwamba waziri huyu bado anayo kazi kubwa kuhakiki­sha maslahi ya wasanii wa Kitan­zania, yanaboreshwa, mikataba ya kinyonyaji wanayoingia wasanii inatafutiwa ufumbuzi haraka na kutatua changamoto mbalimbali zinazowakabili waandishi wa habari, ikiwemo ya vyombo vya dola kutumia nguvu dhidi ya waandishi.

  1. JOYCE NDALICHAKO

Waziri wa Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi Profesa Joyce Ndalichako, ametajwa kuwa anachapa kazi vizuri na ndiyo maana kwa mara ya kwanza baada ya kipindi kirefu kupita, shule za serikali zimeanza kung’ara kwenye kumi bora za matokeo ya mitihani ya kitaifa, ukiwemo ule wa Kidato cha Sita ambapo Shule za Kibaha na Mzumbe zilizitoa kimasomaso shule za serikali.

  1. JENISTA MHAGAMA

Mwanamama Jenista Mhag­ama, Waziri wa Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Walemavu, naye ameingia kwenye orodha hii kutokana na jinsi anavyoshu­ghulikia changamoto mbalimbali zinazoikabili wizara yake.

  1. CHARLES MWIJAGE

Ni Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji, anatajwa kwenda sambamba na kasi ya mheshimi­wa rais ya kuhakikisha ‘Tanzania ya Viwanda’ inatimia.

Jitihada zake mbalimbali za kutengeneza mazingira mazuri ya uwekezaji, kuwatembelea wa­fanyabiashara sehemu mbalim­bali na kuzungumza nao kuhusu changamoto zinazowakabili, pamoja na kuhamasisha ujenzi wa viwanda, ni miongoni mwa sifa zinazombeba.

 

MAKALA: MWANDISHI WETU

Comments are closed.