The House of Favourite Newspapers

Hawa Watapiga Penati, Faulo, Kona

MSIMU mpya wa Ligi Kuu Bara unazinduliwa rasmi leo Jumamosi kwa mchezo wa Ngao ya Jamii ambao utazikutanisha timu za Simba na Azam FC, mchezo ambao utapigwa kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.

 

Baada ya hapo, pazia la ligi kuu litaanza rasmi Agosti 24, mwaka huu katika viwanja tofauti huku kwa sasa timu zikiendelea na maandalizi yao kuelekea msimu huo mpya. Lakini siku zote kwenye timu kubwa na ligi zile kubwa Ulaya na hata Afrika, kumekuwa na utaratibu wao ambao wanajiwekea.

 

Klabu zimekuwa na utaratibu wake ambapo kocha anakuwa na mchezaji wake maalum wa kupiga mipira ile ya kutengwa yaani penalti, faulo na hata kona na asipokuwepo huweza kumpa mchezaji mwingine jukumu hilo. Hili lipo kote.

 

Kama haufahamu, basi makala haya yanakuchambulia wachezaji ambao msimu ujao usije kushangaa utakapoona wanapiga mipira hiyo kwani wao ndiyo wamepewa dhamana hiyo.

1. SIMBA

Msimu uliopita, John Bocco na Meddie Kagere walifanya kazi ya ziada hasa kwenye suala la upigaji wa penalti na kuibeba timu hiyo na kuutwaa ubingwa wa ligi hiyo.

Kikosi hicho kimekuwa kikimtumia John Bocco kama mpiga penalti wao namba moja. Huku upande wa mipira ile ya faulo na kona Mzambia, Clatous Chama ndiye amepewa jukumu hilo.

 

2. AZAM FC

Azam msimu ujao wataendelea kumtumia nahodha wao, Aggrey Morris katika upigaji wa penalti pamoja na faulo ingawa kwa sasa ni majeruhi na yupo nje ya uwanja.

Mbali na Morris, Mudathir Yahya amekuwa akipiga mipira ya faulo na kona.

3. YANGA

Msimu uliopita kwenye kikosi cha Yanga mara nyingi kwenye mipira ya faulo pamoja na kona alitumika Ibrahim Ajibu ameondoka aliyekuwa akisaidiana na Papy Kabamba Tshishimbi.

Msimu huu tangu Mwinyi Zahera aanze kukinoa kikosi chake ambacho kwa kiasi kikubwa ni kipya, amekuwa akimtumia Patrick Sibomana kwenye upigaji wa penalti pamoja na faulo.

4. KMC

Sio wenyeji sana kwenye ligi kuu, lakini uwezo wao ulionekana msimu uliopita. Hawa vijana wa kocha Jackson Mayanja, mpiga penalti wao ambaye wamekuwa wakimtumia mara kwa mara ni Juma Kaseja ambaye ni kipa na Vitalis Mayanga.

Upande wa mipira ya faulo amekuwa akihusika Amos Amos na Mayanga ambaye amesajiliwa msimu huu ndani ya kikosi hicho.
n KLABU zimekuwa na utaratibu wake ambapo kocha anakuwa na mchezaji wake maalum wa kupiga mipira…

5. POLISI TANZANIA

Hii ndiyo kwanza imepanda na itacheza Ligi Kuu Bara kwa mara ya kwanza ikiuwakilisha Mkoa wa Kilimanjaro.

Licha ya ugeni na kocha akiwa bize kutengeneza kikosi chake, Seleman Matola tayari amewapa majukumu nyota wake. Upigaji wa penalti atahusika William Lucian ‘Gallas’ na Marcel Kaheza huyu pia atakuwa anapiga faulo.

 

6. MTIBWA SUGAR

Kikosi hicho ambacho mara nyingi zaidi hutumia vijana kama ambavyo kocha wao ni kijana, lakini kwenye upigaji wa penalti wameona bora hilo jukumu wampe mkongwe Shaban Nditi. Upande wa mipira ile ya faulo, wamewakabidhi vijiti vijana Salum Kihimbwa pamoja na Issa Rashid ‘Baba Ubaya’.

7. KAGERA

Kocha Mecky Maxime ambaye naye kikosi chake kina mabadiliko makubwa tofauti na msimu uliopita, amesema kwa sasa bado hajapata wachezaji sahihi kwa ajili ya penalti, faulo na kona kwani bado anajenga kikosi ila msimu uliopita kwenye penalti alimtumia zaidi Ramadhan Kapela aliyetua KMC.

 

8. MBEYA CITY

Hawa kwa kiasi kikubwa, kikosi chao kimefanyiwa mabadiliko na sasa kipo chini ya kocha Juma Mwambusi. Msimu uliopita mpiga penalti alikuwa ni Mohamed Samatta ambaye kwa sasa yuko KMC, bado wanasaka mrithi wake. Lakini kwa upande wa upigaji wa faulo, wanamtumia zaidi Selemani Mangoma.

 

9. COASTAL UNION

Hawa ni vijana wa Kocha Juma Mgunda. Msimu uliopita kocha huyo alimkabidhi Raizin Hafidhi kupiga penalti zote ambaye kwa sasa yupo Gwambina, hivyo anasaka mrithi. Likija suala la upigaji wa mipira ya faulo, kwake anatumia viungo tofauti wa klabu hiyo kwa sababu asilimia kubwa wanaweza kupiga mipira iliyokufa.

 

10. NAMUNGO FC

Wageni hawa wa ligi wanatoka kwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Kassim Majaliwa kule Lindi.

Wanafundishwa na Kocha Mrundi, Hitimana Thierry tangu wakiwa Ligi Daraja la Kwanza ambapo alikuwa anamtumia Danny Joram Gustavo ambaye kwa sasa ni majeruhi na hivi karibuni kwenye mechi za kirafiki amekuwa akimtumia Luca Kikoti.

 

11. NDANDA FC

Tayari wameanza maandalizi yao lakini mpaka sasa bado katika nafasi hizo hawajapata wachezaji ambao watawatumia sababu bado wanapambana kujenga kikosi chao.

Comments are closed.