The House of Favourite Newspapers

Jerome kula bata jukwaani Yanga

0

Sina-JeromeNa Nicodemus Jonas

KIUNGO Jerome Sina anayefanya majaribio Yanga, ataendelea kubaki katika klabu hiyo pengine hadi katika usajili wa Juni mwakani ndipo jina lake liidhinishwe acheze Ligi Kuu Bara msimu ujao.

Awali Yanga ilimpokea Sina kwa majaribio huku ikipiga hesabu za kumsajili kwa ajili ya mechi za Ligi ya Mabingwa Afrika lakini timu hiyo haikulijumuisha jina lake kwenda Caf.

Badala yake klabu hiyo imepeleka majina ya nyota wake saba wa kigeni na wengine wazawa ili wacheze michuano hiyo inayosimamiwa na Shirikisho la Soka Afrika (Caf).

Kwa mujibu wa Kocha wa Yanga, Hans van Der Pluijm, alisema Sina ameonyesha kiwango kizuri katika majaribio yake na ni aina ya wachezaji anaohitaji, lakini sasa kikwazo kikubwa ni kwamba haruhusiwi kuitumikia timu hiyo.

 “Tumekuwa naye (Sina) kwenye mazoezi muda sasa, lakini siwezi kukuelezea nini kilichopo, ni masuala ya uongozi na mimi pia, lakini Sina ni mchezaji mzuri sana,” alisema Pluijm kwa ufupi.

Licha ya Pluijm kuficha kidogo, lakini gazeti hili linafahamu kuwa, Yanga haitaki kumuachia Sina na imepiga hesabu za kuwa naye msimu ujao huku ikiwa naye kama ilivyokuwa kwa winga Geofrey Mwashiuya aliyesajiliwa kutoka Kimondo FC.

Tayari Sina raia wa DR Congo aliyetupiwa virago Rayon Sports ya Rwanda, amepewa jezi namba saba iliyokuwa inavaliwa kiungo Mbrazili, Andrey Coutinho, ambaye amejiunga na Kwampog ya Korea.

Leave A Reply