The House of Favourite Newspapers

Kaburi la Yesu Lafunguliwa Upya Jerusalem


Timu ya wanasayansi na wakarabati wamekamilisha kazi katika eneo linalodaiwa kuwa ni kaburi la Yesu Kristo katika mji wa zamani wa Jerusalem, na itafunguliwa wazi kwa umma siku ya Jumatano.

Kundi hilo limefanya kazi hiyo kwa muda wa miezi tisa kwenye Kanisa la Mtakatifu Sepulchere na walilenga katika sehemu ndogo ya juu ya kaburi, inayojulikana kama ‘Edicule’.

Waumini wengi wa dini ya kikristo wanaamini kuwa mwili wa Yesu ulizikwa katika eneo lililokuja kuwa Kanisa la Mtakatifu Sepulchre.

Mzozo kati ya madhehebu matatu ambayo kwa pamoja husimamia kanisa hilo likiwemo Kanisa la Kiothodoksi la Ugiriki, Kanisa la Kiarmenia na Kanisa Katoliki la Kirumi ulichelewesha ukarabati huo kwa miongo mingi.

Kazi ilianza mwaka jana baada ya mamlaka ya Israel, ambayo imekuwa ikiiongoza Mashariki ya Jerusalem tokea ilipoiteka katika vita ya Mashariki ya Kati mnamo mwaka 1967, kusema kuwa kanisa hilo siyo salama kwa kuwa chumba hicho kilikuwa kimekuwa dhaifu sana kiufundi.

Aidha, kilikuwa kimechakaa na kubadilika rangi na kuwa karibu rangi nyeusi kutokana na masizi ya mishumaa mingi ambayo huwashwa eneo hilo.

Antonia Moropoulou, aliyesimamia ukarabati huo, amesema chumba hicho sasa kimepata tena rangi yake asili inayokaribia hudhurungi.

Vyombo vya habari vimeripoti kuwa kila dhehebu limechangia mradi huo. Mfalme Abdullah wa Jordan nae alitoa mchango wake binafsi, kazi yote iligharimu takribani dola za kimarekani bilioni 3.3

Comments are closed.