The House of Favourite Newspapers

KAPO ZA MASTAA BONGO ZILIZOBAMBA 2018

WAKATI mwaka wa 2018 ukikaribia kufika ukingoni, kwenye ulimwengu wa mastaa yapo mambo mbalimbali yaliyotokea tangu ulipoanza yakiwemo mazuri na mengine mabaya.  Katika makala hii tunakuletea kapo za mastaa ambazo zimebamba ndani ya mwaka huu na kuwa gumzo kila kona.

KIBA NA AMINA

STAA wa Bongo Fleva, Ali Salehe Kiba mwaka huu ulikuwa mzuri kwake kwani aliachana na ukapera na kuingia kwenye ndoa na mrembo raia wa Kenya, Amina Khalef. Kapo hii imetikisa kutokana na watu kumsifia mwanamke huyo kuwa ni mrembo hivyo wengi kumpongeza Kiba kwa kujua kuchagua.

AY NA REMMY

Februari mwaka huu ilikuwa ni cherekochereko baada ya mwanamuziki Ambwene Yessayah ‘AY’ kufunga ndoa ya kimila huko Rwanda na aliyekuwa mchumba wake wa siku nyingi, Rehema Suddy ‘Remmy’ ambaye ni raia wa nchi hiyo na baadaye sherehe ya harusi kufanyika jijini Dar es Salaam. Wawili hawa walibamba kwenye mitandao mbalimbali ya kijamii hasa kutokana na urembo wa Remmy ambapo hivi karibuni walijaaliwa mtoto wa kiume.

DIAMOND NA TANASHA

Staa wa Afro Pop, Nasibu Abdul ‘Diamond’ na Tanasha Donna Barbieri Okech ‘Zahara Zaire’ ni kapo ambayo imetikisa kwa mwaka huu licha ya kwamba uhusiano wao una muda mfupi lakini kila kona sasa wanajadiliwa. Diamond alitangaza kuwa anatarajia kuingia kwenye ndoa na mrembo Tanasha Februari mwaka ujao, ambapo kabla ya hapo alikuwa kwenye uhusiano na mama wa watoto wake ambaye ni raia wa Uganda, Zarinah Hassan ‘Zari’ lakini wakamwagana na tangu hapo akawa anatajwa kutoka na warembo tofauti akiwemo Lynn na Kim Nana.

LULU NA MAJAY

Uchumba wa staa wa filamu, Elibeth Michael ‘Lulu’ na Francis Shiza ‘Majizo’ umekuwa kivutio kwa wengi ikidaiwa kuwa, wameendana.

Kapo hii imekuwa ikizungumziwa sana kutokana na kwamba Lulu alikuwa kwenye matatizo ya kifungo cha nje alichohukumiwa kutokana na kesi ya kumuua bila kukusudia aliyekuwa msanii maarufu wa filamu, Steven Kanumba ambapo wakati akielekea kumaliza kifungo alichomaliza Novemba mwaka huu, alivishwa pete ya uchumba na mchumba wake huyo.

HAMISA NA JOSH

Mwanamitindo Hamisa Mobeto na Josh Adeyeye ambaye ni raia wa Marekani walikiki vilivyo kwani baada ya kukutana nchini humo ambako Hamisa alikwenda kwa ajili ya kufanya shoo alimnadi mwanaume huyo mitandaoni kwa kuweka picha wakiwa kimahaba. Kutokana na kwamba ilikuwa ni muda mchache tangu Hamisa atangaze kumwagana na baba mtoto wake, Nasibu Abdul ‘Diamond’ kapo hii ilichukua nafasi kubwa sana kujadiliwa na kupongezwa.

Licha ya kuvutia na kuwa gumzo kila kona baadaye ilikuja kugundulika kuwa ilikuwa ni kiki ya wimbo wa Hamisa ambao mwanaume huyo ameonekana kwenye video yake. Mbali na kudaiwa kuwa ni kiki, inaelezwa kuwa, wawili hao wanapeana ‘mambo’ kwa siri kwani jamaa ana mtu wake na Hamisa mbali na projekti yao anaonekana kumzimikia ile mbaya.

Makala: MWANDISHI WETU

Comments are closed.