KIRAKA wa Simba, Shomari Kapombe, ametamka kuwa mipango aliyonayo kocha wao Mfaransa, Pierre Lechantre, anaamini timu yao itachukua ubingwa wa Bara mikononi mwa Yanga na kufika mbali kwenye michuano ya kimataifa.
Kiraka huyo, alirejea uwanjani hivi karibuni na kucheza mchezo wake wa kwanza dhidi ya Kagera Sugar katika Ligi Kuu Bara.
Simba inatarajiwa kucheza mchezo wake wa kwanza wa Kombe la Shirikisho Afrika dhidi ya Gendermerie Tnale ya Djibouti wiki hii kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar.
Akizungumzia mchezo huo, Kapombe alisema kuwa kikosi chao kipo fiti na tayari kwa ajili ya mchezo huo ambao wanahitaji kushinda michezo yao yote miwili ya nyumbani na ugenini ili wafike mbali katika michuano hiyo.
Kapombe alisema, kocha wao Mfaransa hivi sasa anawaongezea baadhi ya vitu muhimu ikiwemo mbinu za jinsi ya kushambulia goli lao wakati wakiwa hawana mpira.
“Kocha wetu ana mipango mizuri katika kuelekea kwenye michuano ya kimataifa ambayo anataka kuona timu yetu ya Simba inafika mbali na kutengeneze historia ambayo haitaweza kusahulika.
“Na hilo linawezekana kutokana na mbinu, pia mfumo mpya aliouingiza katika timu ambao utaipa timu yetu mabao mengi kama tukiushika wachezaji na kuufanyia kazi katika mechi.
“Malengo ni kufika mbali katika michuano hiyo na kikubwa tunachotakiwa kukifanya hivi sasa ni kushinda mchezo wetu wa kwanza wa hapa nyumbani ambao utatujengea hali ya kujiamini na kushinda michezo mingine inayofuata,” alisema Kapombe.
Wilbert Moland, Dar es Salaam
Comments are closed.