The House of Favourite Newspapers

Kaze Aanza na Pacha ya Fiston…

0

 

KOCHA Mkuu wa Yanga, Mrundi Cedric Kaze ameweka wazi kuwa kwa sasa kitu ambacho anakifanya ni kutengeneza muunganiko wa wachezaji wake wapya wakiwemo Saidi Ntibazonkiza ‘Saido’ na Fiston Abdoul Razak.

 

Kocha huyo ameongeza kuwa anataka kufanya hivyo kwa ajili ya kufanya vizuri kwenye mechi zao za mzunguko wa pili ambazo zitakuwa ngumu kuliko zile zilizopita.

 

Katika usajili wa dirisha dogo, mabosi wa Yanga waliwasajili Saido, Fiston na Dickson Job, ikiwa ni kwa mujibu wa mapendekezo ya Kaze kwa ajili ya kufanya vizuri katika mechi za Ligi Kuu Bara.

 

Kocha huyo ameliambia Championi Jumatano, kuwa kwa sasa kitu ambacho atakifanya kwa haraka ni kuhakikisha anasuka muunganiko kati ya wachezaji hao wapya sambamba na wale ambao walikuwepo awali.

 

“Kwa sasa nataka tupate muunganiko wa wachezaji hawa wapya ambao wamesajiliwa na wale wenzao ambao walikuwepo tangu mwanzo.

 

“Nataka waunganike na wenzao mapema kabla ya mechi zetu za mzunguko wa pili kuanza ambazo zitakuwa ngumu zaidi kuliko zile ambazo tulicheza awali. “Ikiwa wataelewana mapema na wenzao itakuwa faida kwetu kwa ajili ya kujihakikishia nafasi ya kupata matokeo mazuri,” alimaliza Kaze.

 

Fiston ambaye anatajwa kuwa mmoja kati ya washambuliaji mahiri atakuja kuungana na Saido ambaye ameshazoea mikikimikiki ya Yanga akiwa amefunga mabao matatu kwenye michuano yote kwenye timu hiyo.

Stori: Said Ally, Dar es Salaam

Leave A Reply