The House of Favourite Newspapers

KELELE NYINGI ZINAPOTEZA UELEKEO

  HALOOO ehhhh tena ya kisoda ati! Miye kama kichwa vile, usiponinyoa utanisuka! Nimeingia tena ustake kuniuliza leo nimefurahi nini! Shoga unitue kama maji yaliyobebwa bila ngata, upo?

Jumatano ile uliokuwa ukiisubiri kumsoma Anti Naa ndiyo hii sasa! Siyo unatumbua macho kama umejaribu nguo iliyokosea kuwekwa vishikizo! Heee heeeiyaaaaa, unalo bibiye! Mchana unalala usiku unaingia kazini, kwa nini usigombane na mwenye nyumba? Watoto wa mjini wanasema raha jipe mwenyewe, ndiyo najipa tena japo ukurasa wenyewe napewa mdogo lakini nawaambia hivi, mwaka huu tutabanana hapahapa mpaka jelo useme jela, upo!

Shoga leo nipo na weweeeeee mwanamama unayemchukulia poa binti yako! Kutwa kumkosesha raha, mtoto anashindwa hata kupumua! Akificha uhusiano wake kutwa kumsema, akiwa na mabwana wengi napo unamsema, shuuutuuuuu! Katembee nao wewe sasa!

Nasema haya siyo kama nimechanganyikiwa, nina akili zangu timamu kabisaaaa maana ninayoandika hapa kila siku huwa nayashuhudia na mengine nasimuliwa, upo?

Ujue kuna umri ukifika watoto wetu hawa wa kike umri unaowaruhusu kuwa na uhusiano huwa wanapata tabu sana! Kutwa wanavunjwa moyo na wazazi wao badala wafarijiwe na kupewa njia sahihi. Akifanya kosa kidogo, utasikia wanaanza kuambiwa maneno mabaya mara; ‘ohhh hivi wewe una nuksi…mbona wenzio wanaolewa wewe upoupo tu hapa, kushinda kupika na kufua minguo yako…’

Tena unakuta anafoka kabisa na kusema kwa sauti kubwa mpaka majirani wanasikia, shoga unadhani majirani hao ambao wengi wao vijana tena wa kiume wakisikia maneno hayo watanyamaza? Watashindwa kutumia fursa?

Ngoja nikung’ate sikio haswaaaa wewe unayeropoka maneno ya ajabu kwa binti yako! Kwanza unamkosesha furaha, vijana wa uswazi wakisikia kauli hizo wanatumia mbinu hiyo unayomwangamiza binti yako kama fursa, matokeo yake binti yako anatapatapa, anatafuta mchumba ambaye atakuja muoa ili tu akufurahishe asiendelee kuishi hapo na wewe.

Huko akipata kijana unafikiri atakuwa sahihi, atakuwa anadanganywa tu na yeye yupo tayari kukubali akufurahishe, hata akiambiwa nitakuoa kabla mwaka kuisha, tena anaweza akawa anatumia njia ya kutoroka na kulala kwake kabisaaaa!

Shoga niyasemayo yapo! Unamkuta binti ameshavurugika akili, ametukanwa na kudharauliwa vya kutosha na mama yake, wee unafikiri ataachaje kujitoa muhanga kwa mwanaume aliyemtongoza siku hiyohiyo na kuishi naye! Tena wengine wanajitoa kama wameolewa, watamtandikia huyo mwanaume, watamfulia, watamtekea maji na kupika juu!

Akipata mimba, mama ndiyo wa kwanza domo kuvimbisha, shuuuutuuuuu! Ulivyomsema ulitaka akaonane na jiwe? Badilika mwanamke wewe, binti yako siyo wa kumpa maneno ya hovyo, ya kumkatisha tamaa! Siku hizi mwenzangu vishawishi vingi na maisha yalivyo ukimpigia kelele nyingi lazima apoteze uelekeo, ajikute anampata mwanaume kukuridhisha usiwe kidomodomo!

Shoga naomba niishie hapa, ni Mimi Anti Naa Shangingi Mstaafu.

Comments are closed.