
RAIS mstaafu Jakaya Kikwete ameteuliwa na Baraza la Wakimbizi Duniani (WRC) kuwa Mwenyekiti-Mwenza katika idara yake ya utendaji ambapo Mwenyekiti wake ni waziri wa zamani wa Mambo ya Nje, Lloyd Axworthy.
Baraza hilo huru linajumuisha viongozi na wataalam mbalimbali duniani ambapo lengo lake ni kutafuta na kuendeleza ufumbuzi mbalimbali unaohusiana na matatizo ya wakimbizi.
Taarifa iliyotolewa na baraza hilo inasema kwamba Hina Jilani wa Pakistan na Rita Süssmuth wa Ujerumani watakuwa pia wenyeviti-wenza pamoja na Kikwete ambapo Paul Heinbecker atashika nafasi ya unaibu na Fen Hampson atakuwa mkurugenzi.
Pia taarifa hiyo iliongeza kwamba, miongoni mwa mambo mengine, baraza hilo litatoa ushauri kuhusianana mabadiliko mapya ya kuimarisha mfumo wa kushughulikia masuala ya wakimbizi duniani.
“Baraza litaanzisha mabadiliko ya kuhakikisha kwamba ushirikiano wa kimataifa kuhusiana na wakimbizi unatabirika na wa kukubalika pande zote,” inasema taarifa hiyo na kuongeza kwamba baraza hilo litakuwa na washauri 17.
“Wakati mgogoro nchini Syria unaingia mwaka wa sita, na matatizo mengine yakijitokeza barani Afrika na duniani, mfumo wa sasa wa kuwalinda wakimbizi unapigania kulinda mahitaji ya nchi husika na wakimbizi pia.
“Hivi sasa ni muhimu zaidi kuwepo kwa mipango thabiti zaidi kuhusu tunavyoweza kuimarisha ushirikiano wa kimataifa na kuhakikisha matokeo bora kwa wakimbizi na mataifa husika, ” alisema Axworthy.

