The House of Favourite Newspapers

Kisa TFF, Wagombea 28 Wafutwa Uanachama Yanga

Viongozi wa matawi ya Yanga wakiongea.

JUMLA ya wanachama 28 wanaogombea nafasi za uongozi wa Klabu ya Yanga, wanatarajiwa kufutwa uanachama kutokana na kosa la usaliti la kwenda kuchukua fomu Shirikisho la Soka Tanzania (TFF).

 

Wagombea hao waliojitosa kuwania nafasi ya uongozi ni ile ya Mwenyekiti, Dk Jonas Tiboroha, Yono Kevela, Mbaraka Igangula na Erick Ninga.

 

Nafasi ya umakamu mwenyekiti ni Titus Osoro, Salum Magege Chota na Yono Kevela wakati wajumbe ni Hamad Ally Islamu, Benjamin Jackson Mwakasonda, Sylvester Haule, Salim Seif, Musa Katabaro, Shftu Amri na Said Baraka.

Wengine ni Pindu Luhoyo, Dominick Francis, Seko Jihadhari, Ally Omary Msigwa, Arafat Ally Haji, Geofrey Boniphace Mwita, Frank Kalokola, Ramadhan Said, Leonard Marango, Bernard Faustin Mabula, Christopha Kashiririka, Athanas Peter Kazige na Faustin Peter Bisangwa.

 

Maamuzi hayo ya kuwaondoa uanachama wagombea hao yalitolewa jana kwenye kikao cha viongozi wa matawi ya kanda tano waliokutana juzi Jumatatu kwenye Makao Makuu ya klabu hiyo iliyopo Jangwani jijini Dar es Salaam.

 

Akizungumza na Championi Jumatano, Mwenyekiti wa Kanda ya Kinondoni ambaye pia ni Katibu wa Tawi la Manzese, Shabani Uda alisema kuwa kitendo kilichofanywa na wanachama hao kwenda kuchukua fomu za uchaguzi TFF ni usaliti.

“Tumekutana hapa kujadili masuala mbalimbali ya klabu yetu na kubwa tunajadili hili lililopo mbele yetu, juu ya uchaguzi tunaotaka tuusimamie sisi wenyewe na siyo TFF.

 

“Kiukweli kabisa tuseme kuwa, hakutakuwa na mwanachama yeyote atakayejitokeza siku hiyo ya uchaguzi waliyoipanga kama TFF wakiendelea kusimamia uchaguzi wetu, ni vema wakalifahamu hilo.

 

“Kwa kuanza tunaanza na hao wanachama waliokwenda kuchukua TFF kwa ajili ya kugombea nafasi za uongozi wa Yanga kwa kuwasimamisha uanachama kabla ya kwenda kwenye uchaguzi wetu mkuu wa dharura tuliouomba, kwani hicho kitendo walichokifanya ni cha usaliti,” alisema Uda.

Comments are closed.