Korea Kaskazini Yajipanga Kutumia Zana za Nyuklia Kwenye Uwanja wa Vita
RAIS wa Korea Kaskazini Kim Jong Un ameagiza maafisa wa jeshi la nchi hiyo kuandaa mipango ya kuimarisha vikosi vya mbele kwenye mapambano ya uwanja wa medani kuwa na silaha imara na angamizi.
Kwa mujibu wa shirika la utangazaji la nchi hiyo Korean Central News Agency(KCNA) limeitafsiri kauli hiyo kama kichocheo cha matumizi ya nyuklia kwenye vikosi vya mbele vya mapigano katika uwanja wa medani.
Shirika hilo limebainisha kuwa kauli ya Rais Kim imekaa kimkakati kwani hajatamka wazi kwa maafisa wa jeshi kutekeleza mpango wa kuimarisha vikosi vya mble vya mapigano kwa njia gani lakini wachambuzi wa masuala ya kivita wamebainisha kuwa kauli hiyo inaidhinisha matumizi ya zana za nyuklia kwenye uwanja wa medani.
kumekuwa na mvutano mkubwa wa kisiasa kati ya nchi ya Korea Kaskazini pamoja na Korea Kusini, mvutano ambao umedumu kwa miaka mingi sasa ambao unapelekea mataifa hayo mawili kuendelea kutishiana usalama karibu kila siku.
Naye Jeffrey Lewis Mkurugenzi wa Programu ya kuzuia kuenea kwa matumizi ya nyuklia upande wa Asia Mashariki ambaye anatoka katika chuo kikuu cha Middlebury kinachojihusisha na masomo ya kimataifa kilichopo nchini Marekani ameandika kupitia mtandao wake wa Twitter akisema kuwa kitendo cha Rais Kim kukaa kikao hicho na maafisa wa juu wa jeshi ni kurasmisha matumizi ya zana za nyuklia kwenye vikosi vya mbele vya mapigano katika uwanja wa medani