The House of Favourite Newspapers

Kujiuzulu Kwa Manji Yanga… Mzee Akilimali Amefunguka

0

MANJI NA AKILI MALI (1)

WAKATI vichwa vya habari nyingi za michezo hapa nchini zikizungumzia kuhusu sakata la Mwenyekiti wa Klabu ya Yanga, Yusuf Manji, kudaiwa kujiuzulu nafasi yake hiyo, taarifa ambazo zilianza kusambaa jana kwenye mitandao ya kijamii na baadhi ya vyombo vya habari, mwanachama mkongwe wa klabu hiyo, Ibrahim Omary Akilimali maarufu kwa jina la Mzee Akilimali ametoa kauli tata juu ya sakata hilo.

Ikiwa mpaka sasa Manji hajatoa tamko lolote juu ya uamuzi wake huo wa kujiuzulu,  Mzee Akilimali amenukuliwa akisema kuwa kuna watu wa Yanga wamemuita ili kuzungumza kuumaliza mvutano unaoendelea ambapo inaelezwa kuwa mzee huyo amechangia maamuzi ya Manji kujiondoa Yanga kutokana na kumshutumu kwa maneno mengi.

Akihojiwa na kituo cha Radio cha EFM, leo asubuhi Mzee Akilimali alinukuliwa akisema: “Msitake kuyakuza haya mambo, subirini kwanza nataka tuyamalize, mimi wameniita ndiyo maana nipo huku ili kuyamaliza.”

Alipoulizwa yupo wapi na ameitwa na nani, Akilimali alisema: “Nimekwambia nimeitwa huku, wewe subiri kwanza tuyamalize kisha utanipigia, subiri baada ya nusu saa nitakubeep unipigie.”

Licha ya kuendelea kubanwa kufafanua zaidi juu ya kinachoendelea, mzee huyo alisisitiza kuwa apigiwe baadaye na kukata simu.

Taarifa zaidi zimeeleza kuwa Mzee Akilimali ameibuka na kutoa ufafanuzi wa mambo kadhaa ikiwemo kuomba radhi kwa kauli zake.

Baadaye alipopigiwa simu mzee huyo alisikika kama mtu ambaye amepoa na kuwa mpole ambapo alisema anawaomba radhi Wanayanga kama atakuwa amewakosea kwa kauli zake lakini nia yake ni kuitaka Yanga iwe moja na Manji aonyeshe heshima kwa wazee wa klabu hiyo.

“Manji ni kijana wetu, sisi wazee nikiwemo mimi tulichangia yeye kuingia ndani ya Yanga, hata mimi ndiye niliyemkabidhi ngao ya uchifu wa Yanga, sasa hapo katikati alikuwa hatushirikishi sisi wazee kama ilivyokuwa zamani.

“Akawa anafanya maamuzi anayoyajua yeye, nia yetu sisi wazee ni kuifanya Yanga iwe moja kuwe na mshikamano, unajua Manji ametutoa mbali, sisi ni Yanga moja, kwa mapenzi yangu yote nataka Yanga iwe kitu kimoja. Yanga ni moja na hakuna mpasuko,” alisema Mzee Akilimali.

Mzee Akilimali ni mzaliwa wa Kigoma, ambapo anadai alianza kuipenda Yanga tangu miaka ya 1950.

Leave A Reply