Kwa Wiki ya Kwanza tu Muvi ya Maisha ya Tupac Yapiga Bilioni 53
Habari ndiyo hiyo! Huku ikiwa imetimiza wiki tangu filamu inayohusu maisha ya nguli wa Hip Hop nchini Marekani, Tupac Shakur iitwayo All Eyez On Me kuingia sokoni, tayari filamu hiyo imejizolea kiasi cha dola milioni 25.4 katika wikiendi ilipokuwa ikionyesha.
Filamu hiyo ambayo imezua gumzo kubwa huku baadhi ya wasanii wakionekana kuiponda wakiwemo 50 Cent, Jada Pinkett, imekuwa kivutio kwa watu wengi kwani asilimia kubwa walitamani kuona maisha ya msanii huyo yaliyoigizwa na muigizaji anayechipukia, Shipp Jr ambaye anafanana mno na Tupac.
Filamu hiyo ilitengenezwa kwa dola milioni 45 ambazo ni zaidi ya bilioni 90 kwa pesa za madafu. Kwa wikiendi iliyopita, filamu hiyo ilishika nafasi ya tatu huku nafasi ya kwanza ikishikwa na Cars 3, Wonder Woman ambayo kwa ujumla ndiyo inayoongoza kwa filamu mpya zilizoingiza kiasi kikubwa cha pesa ambapo mpaka sasa imeingiza dola milioni 275 ambazo ni zaidi ya shilingi bilioni 500. Ila kwa wikiendi hii, All Eyez On Me imetisha sana.
Na: Nyemo Chilongani