Dar es Salaam 23 Novemba 2023: Kampuni ya mafuta ya Lake Energies ni miongoni mwa makampuni yaliyojitokeza kudhamini Tuzo za Filamu Tanzania mwaka huu 2023 zinazotarajiwa kufanyika desemba 16 mwaka huu.
Akizungumza kwenye hafla ya kutajwa majina ya walioteuliwa kwenye vipengele mbalimbali vya tuzo hizo, Meneja Masoko na Mawasiliano wa Lake Energies Tanzania, Matina Nkurlu amesema kampuni hiyo imeamua kujitosa kwenye kudhamini tuzo hizo katika kumsapoti Rais wa Jamhuri Ya Muungano wa Tanzania, Dk. Samia Suluhu Hassan ambaye amekuwa pega kwa bega na wasanii na wanamichezo kwa ujumla.
Meneja Masoko wa na Mawasiliano wa Lake Energies ambao ni moja ya wadhamini wa Tuzo za Filamu Tanzania mwaka huu, Matina Nkurlu (kulia) akifuatiwa na msanii wa vichelesho Lucas Mhuvile maarufu Joti (mwenye tai) na Meneja Uhusiano wa Airtel Tanzania, Jackson Mmbando kulia ni mmoja wa wadau waliojumuika kuhudhuria hafla ya kutangazwa washiriki wa Tuzo la Filamu hapa nchini.
Katika hafla hiyo mgeni rasmi alikuwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Sanaa Utamaduni na Michezo, Gerson Msigwa ambaye aliwasisitiza wasanii kuzidi kuongeza ubunifu kwenye fani hiyo na kuwaambia kuwa Rais Dk Samia yuko pamoja nao.
Katika kumalizia Msigwa aliwapongeza wadhamini wote waliojitokeza kudhamini tuzo hizo na kusema kuwa udhamini huo unaongeza chachu na kunogesha tuzo hizo. HABARI/PICHA NA RICHARD BUKOS/ GPL