The House of Favourite Newspapers

Maadhimisho ya Siku ya Mtoto Afrika; TAMWA Yaitaka Jamii Kuheshimu Haki ya Mtoto

0

Watanzania leo wanaungana na dunia nzima kuadhimisha Siku ya Mtoto wa Afrika, maadhimisho ya siku hii yalianza mwaka 1991 baada ya kuteuliwa na Umoja wa Afrika katika kuenzi michango ya watoto walioshiriki maandamano Mjini Soweto, Afrika Kusini mwaka 1976 pamoja na kujengea jamii uelewa juu ya umuhimu wa elimu bora kwa watoto.

Kauli mbiu ya maadhimisho haya kitaifa kwa mwaka huu ni “Zingatia Usalama wa Mtoto katika Ulimwengu wa Kidijitali” kauli mbiu hiyo inasisitiza kuwalinda watoto na kuwaongoza kwenye matumizi ya kidijitali ikiwemo simu za mkononi, kompyuta na runinga kwa kuwa vikitumika vibaya vinaweza sababisha ukatili wa mitandaoni kwa watoto.

Siku ya Mtoto wa Afrika hutumika kuwakumbusha watoto wetu hatua ya kijasiri waliyoichukua wenzao huko Afrika Kusini katika kulinda haki zao. Watoto wanakumbushwa kwamba wanaweza kuleta mabadiliko hata wakiwa wadogo.

Kwa hivyo, Siku Ya Mtoto wa Afrika inaadhimishwa kwa maslahi mapana ya watoto wa Afrika na inapaswa sisi watu wazima kujitolea kwa hali na mali katika nafasi zetu ili kushughulikia changamoto nyingi zinazokabili watoto katika bara zima na hasa hapa nyumbani Tanzania.

Chama cha Wanahabari Wanawake Tanzania (TAMWA) katika kuadhimisha siku hii, tunatoa rai kwa jamii kuweza kuongeza ulinzi kwa watoto kwa kuwakinga na vitendo vya ukatili dhidi yao ikiwemo ukatili wa mitandaoni, mimba za utotoni, ndoa za utotoni, ulawiti, ubakaji, ukeketaji, unyanyapaa na ajira za watoto.

TAMWA kupitia tamko hili ambalo ni sehemu ya maadhimisho, kinamtaka kila mtu kwenye jamii kuwa chachu ya kutengeneza mazingira rafiki kwa watoto kuweza kutoa taarifa endapo ataona viashiria vya ukatili vinavyofanywa na mtu yoyote katika mazingira atakayo kuwepo mtoto ikiwemo ya mitandaoni.

Licha ya kuwepo kwa msukumo wa mabadiliko ya teknolojia yanayopelekea watoto kuhamasika kutumia simu za mkononi, compyuta na runinga katika kupata taarifa, ni jukumu la kila mtu kuwafundisha watoto matumizi sahihi ya mitandao ya kijamii, pamoja na kuwepo kwa mazingira stahiki ili kuwalinda na ukatili ikiwemo udhalilishaji wa kimtandao.

Katika mkataba wa haki za mtoto duniani uliopitishwa na Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa miaka 30 iliyopita umeonesha dhahiri unayosimamia zaidi nguzo kuu nne ambazo ni haki ya kutobaguliwa, kuhakikisha mahitaji yake yanatimizwa, haki ya kuishi na kuendelezwa na haki ya kusikilizwa hivyo hatuna budi kuhakikisha tunatekeleza hilo.

Katika hali isiyo ya kawaida, nyumbani, shuleni, barabarani pamoja na nyumba za ibada zimekuwa ni sehemu zinazoripotiwa kwa vitendo vya ukatili na unyanyasaji dhidi ya watoto huku wanaokabidhiwa jukumu la kumlinda mtoto wakiwa ndio watuhumiwa wa matukio hayo wakiwemo wazazi, walimu, walezi, ndugu pamoja na majirani.

Kwa mujibu wa Takwimu za Wizara ya Mambo ya Ndani nchini Tanzania kutoka Julai 2022 hadi Mei 2023, jumla ya mashauri 14,184 ya matukio ya Ukatili wa kijinsia kwa Watoto yalitolewa taarifa katika Vituo vya Polisi ikilinganishwa na matukio 12,642 yaliyotokea Mwaka 2021/22.

Aidha, Katika Hotuba ya Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Dkt. Dorothy Gwajima alisema “kuanzia Januari 2022 hadi Machi 2023 jumla ya matukio ya Ukatili 15,901 yaliripotiwa Polisi. Kati ya matukio hayo Kesi 671 ndiyo zilifikishwa Mahakamani ambapo 368 zilizotolewa hukumu na kesi 303 zinaendelea”.

Aidha pengine kwa kuongezeka kwa matukio haya inadhihirisha kuwa kuna muamko kwenye jamii katika kuripoti masuala ya ukatili kwa watoto au pengine ni ongezeko la ukatili limezidi na si kwakuwa kuna mwamko wa jamii katika kuripoti matukio hayo.

TAMWA tunatoa wito kwa jamii kuendelea kufichua vitendo hivyo katika vyombo vya usalama ili kutokomeza matukio hayo dhidi ya watoto kwani mtoto wa mwenzio ni wako.

“Kutokomeza ukatili dhidi ya watoto ni jukumu la kila mtu na tusiruhusu mtoto wa kike kupoteza fursa ya elimu na kufurahia utoto wake kwa kumlazimisha kuingia katika ndoa akiwa na umri mdogo pia ni ukiukwaji wa haki za binadamu, hivyo tunaihimiza Serikali kufanyia marekebisho sheria zote zinazokandamiza ustawi wa watoto ikiwemo sheria ya ndoa ya mwaka 1971”. Dkt Rose Reuben.

“Ndoa za utotoni ni suala la afya pamoja na ukiukwaji wa haki za binadamu, kwani wasichana walioolewa kwa umri mdogo wana uwezekano mkubwa wa kuathiriwa na fistula na vifo vya kina mama” Dkt Rose

Licha ya juhudi za Tanzania kukomesha ukatili dhidi ya watoto, uelewa kuhusu kinga na mikakati kwa ujumla hautoshi. Ukatili dhidi ya watoto umefichua athari kubwa katika vipengele vya msingi vya afya ya kihisia, kitabia, na kimwili pamoja na maendeleo ya kijamii katika maisha yote na hasa katika mazingira ya elimu ambapo ujuzi wa mtoto unakuzwa.

TAMWA tunatoa wito kwa serikali yetu sikivu, jamii ya watanzania na wadau wote kushirikiana katika kushughulikia matukio ya vitendo vya ukatili dhidi ya watoto ambayo yanaendelea kushamiri kwa kasi kubwa hapa nchini na duniani kote kama tunavyoshuhudia kupitia vyombo vya habari na mitandao ya kijamii.

Katika kumlinda mtoto wa afrika TAMWA tunaomba ushirikiano wa wadau wote wakiwemo wazazi, walezi, wanasheria, serikali kwa ujumla, wadau wa maendeleo kushirikiana kwa pamoja ili kuhakikisha ulinzi na usalama wa watoto wetu ni wa uhakika na endelevu.

“TAMWA tunampongeza Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan pamoja na Waziri mwenye dhamana, ambao wanaonesha wazi kuwa wanasimamia vyema haki za watoto, tumewaona na kuwasikia wakipinga ukatili kwa watoto hatuna budi kusimama nao katika hili “ Dkt Rose Reuben

Leave A Reply