The House of Favourite Newspapers

Mabosi wapya Yanga wana kasi ya ajabu

KAMATI mpya ya kuisimamia timu ya Yanga, imeahidi kutoshuka kileleni katika msimamo wa Ligi Kuu Bara huku wakiahidi kurejesha kasi yao ya ushindi kwenye michezo ijayo ya Ligi Kuu Bara na Kombe la Shirikisho wakianza na Alliance United ya Mwanza.

 

Hatua hiyo imejulikana ikiwa ni saa chache tangu kamati hiyo mpya kuteuliwa na Mwenyekiti wa Bodi ya Udhamini ya Yanga, George Mkuchika ambaye ni Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma.

Mkuchika aliitangaza kamati hiyo mpya ikiwa ni saa chache mara baada ya bodi hiyo kufanya kikao na Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo nchini Tanzania, Dk Harrison Mwakyembe na kufikia baadhi ya makubaliano ikiwemo la kupendekeza uchaguzi mkuu wa Yanga utakaofanyika Aprili 28, mwaka huu.

 

Akizungumza na Championi Ijumaa, Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Lucas Mashauri alisema wana mikakati mikubwa waliyoiweka baada ya kuchaguliwa kuiongoza timu hiyo, kwanza ni kuhakikisha hawapotezi kila mchezo watakaocheza.

 

Mashauri alisema hilo linawezekana kwao kutokana na kamati yao kuongozwa na watu wa mpira ambao ni Said Mtimizi, Hussein Nyika, Hussein Ndama, Moses Katabaro, Abdallah Bin Kleb na Maulid Kitenge.

 

Aliongeza kuwa, kamati yao ambayo imeundwa maalum wakati huu ambapo timu haina uongozi wa juu, pekee kufanya kazi hawataweza, hivyo ameomba ushirikiano kutoka kwa mashabiki wa Yanga kutoka kwenye kila mkoa ili kufanikisha malengo yao.

 

“Kamati yetu mpya iliyochaguliwa na Mkuchika itaanza kufanya kazi rasmi kwenye mchezo wetu wa Kombe la Shirikisho Afrika tutakapocheza na Alliance United.

 

“Tunafahamu wapinzani wetu wamejiandaa, niseme kuwa na sisi tumejiandaa kama kamati kwa kushirikiana na wachezaji, benchi la ufundi kuhakikisha tunawafunga Alliance na kwenda hatua inayofuata ya michuano hiyo.

 

“Hiyo ni kwa kuanza tu, pia tumepanga kuendelea kubaki kukaa kileleni kwenye msimamo wa ligi ili mwishoni mwa ligi tuuchukue ubingwa wa ligi na mwakani tushiriki michuano ya kimataifa,” alisema Mashauri.

 

Mipango yao hiyo ya ubingwa inamaanisha watawapa wakati mgumu wapinzani wao wa jadi, Simba ambao nao kitakwimu wapo vizuri katika mbio za kuwania ubingwa huo wa Ligi Kuu Bara.

Stori: Wilbert Molandi, Dar es Salaam

Comments are closed.