The House of Favourite Newspapers

Nyumba ya Mtoto wa Mbowe Kupigwa Mnada, Mahakama Yateua Madalali

0

MAHAKAMA Kuu ya Tanzania Divisheni ya Kazi imetoa amri na kumteua dalali wa kukamata nyumba ya mtoto wa Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe, Dudley Mbowe na kuipiga mnada kwa kushindwa kulipa Sh milioni 62.7 za waandishi wa habari.

Uamuzi huo wa mahakama umetolewa jana mbele ya Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, Mary Mrio baada ya kupitia hoja za washinda tuzo katika Tume la Usuluhishi na Uamuzi(CMA) Julai 2023.

Shauri hilo namba 28461 la mwaka 2023, wadai Maregesi Paul na wenzake tisa dhidi ya Mkurugenzi wa Gazeti la Tanzania Daima, Dudley Mbowe.

Akiwasilisha hoja mahakamani, Maregesi alidai Mkurugenzi Dudley baada ya wadai kushinda shauri alikubali kulipa lakini baadae hakutekeleza makubaliano.

” Amekaidi kutulipa tumeona njia sahihi tumekubaliana tukamate nyumba yake namba 9 iliyopo Mtaa wa Feza , Mikocheni B barabara ya Chipaka,”alidai Maregesi.

Akitoa uamuzi Naibu Msajili Mrio, alisema mahakama inatoa amri ya kukamata nyumba namba tisa, iliyopo Mtaa wa Feza, Mikocheni B.

“Mahakama inatoa amri ya kukamata nyumba na imemteua Dalali wa Mahakama, Jesca Massawe kutoka Kampuni ya Udalali ya MM Auctioneer &Debt Collectors,”alisema.

Baada ya uamuzi huo, mahakama iliahirisha shauri na kulipanga Machi 4 mwaka huu kwa ajili ya kupata taarifa ya utekelezaji wa amri hiyo

Walalamikaji hao walipata tuzo Julai 17 mwaka 2023 mbele ya Mwenyekiti wa CMA, Bonasia Mollel.

Madai ya awali yalikuwa jumla ya Sh milioni 114 baada ya kukaa mezani kwenye majadiliano kwa pamoja kiwango hicho cha fedha kilishuka na kufikia Sh milioni 62.7.

Dudley alikubali kulipa fedha hizo kwa awamu tatu, Oktoba 30, Desemba 30 mwaka 2023 na awamu ya mwisho ilikuwa Februari 30 mwaka huu lakini hakulipa.

Katika kutafuta ufumbuzi wa suala hilo, Mwenyekiti wa Chadema Freeman Mbowe aliwaita wahariri wa Gazeti la Tanzania Daima ambao ni miongoni mwa wadai nyumbani kwa wakurugenzi wa Gazeti hilo, Dudley na Lilian Mtei.

Wahariri waliokutana na Mbowe Desemba 20 na 21 mwaka jana ni Maregesi, Fidelis Felix, Arodia Peter na Exuperius Kachenje, katika majadiliano hayo, Mbowe alikubali kulipa madai ya wafanyakazi hao mwishoni Desemba lakini hakufanya hivyo hadi sasa.

Leave A Reply