MAJALIWA: SERIKALI ITAENDELEA KUSHIRIKIANA NA UNHCR
SERIKALI ya Tanzania itaendelea kushirikiana na Shirika la Kuhudumia Wakimbizi la Umoja wa Mataifa (UNHCR) katika kutatua changamoto zinazotokana na uwepo wa wakimbizi nchini na kutafuta suluhu ya kudumu kwenye nchi zao ili wakimbizi hao waweze kurejea makwao kuendelea na shughuli za maendeleo.
Kauli hiyo imetolewa na Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa leo (Ijumaa, Agosti 30, 2019) katika mazungumzo yake na Kamishna Mkuu wa UNHCR, Filippo Grandi, kwenye Kituo cha Maonyesho cha Yokohama nchini Japan baada ya kuhitimishwa kwa Mkutano wa Saba wa Kimataifa wa Tokyo kuhusu Maendeleo ya Afrika (Tokyo International Conference on African Development – TICAD 7).
Katika mazungumzo hayo, Waziri Mkuu amesisitiza umuhimu wa UNHCR kuisaidia mikoa inayokaliwa na wakimbizi kutokana na kuharibiwa kwa mazingira.
“Hata hivyo, Serikali ya Tanzania itaendelea kushirikiana na UNHCR kuimarisha ulinzi wa maeneo ya wakimbizi ili wananchi wa maeneo hayo waendelee kuishi kwa amani na utulivu,” alisema.
Naye Grandi amesema amefurahishwa na utayari wa Serikali ya Tanzania katika kupokea wakimbizi na usikivu wa Rais John Magufuli katika kushughulikia changamoto za wakimbizi.
Majaliwa yupo Japan akimwakilisha Rais Magufuli kwenye TICAD 7 ambao umehitimishwa leo akiwa ameambatana na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika ya Mashariki, Profesa Palamagamba Kabudi na viongozi mbalimbali kutoka Serikali ya Muungano na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.
Comments are closed.