The House of Favourite Newspapers

Majembe Mapya Yanga Yafichwa Hoteli ya Kishua

MASTAA wa Yanga kutoka nje ya nchi tayari wameripoti katika timu hiyo na kufikia hoteli ya kishua ya The Atriums iliyopo Africasana jijini Dar es Salaam.

 

Wachezaji hao walioripoti hadi kufikia jana Jumapili ni Issa Bigirimana, Patrick Sibomana, Maybin Kalengo na Mustapha Selemani.

 

Nyota hao wameripoti haraka kwenye timu hiyo kwa ajili ya kuanza maandalizi ya msimu mpya wa ligi ambayo wamepanga kwenda kuyafanyia mkoani Morogoro ambako wataweka kambi.

 

Kwa mujibu wa taarifa ambazo Championi Jumatatu limezipata na kuthibitishwa na Bigirimana, zinasema tayari wapo nchini na kufikia katika hoteli hiyo wakisubiria kambi ya pamoja ya timu hiyo inayotarajiwa kuwekwa wiki hii.

 

Bigirimana alisema kuwa, amejipanga vema kwa ajili ya msimu mpya wa ligi na kikubwa anaahidi kuifanyia makubwa timu hiyo katika kuelekea msimu ujao wa ligi.

 

“Tupo tumefikia The Atriums Hotel tukisubiria kambi ya pamoja ya timu ambayo huenda ikaanza wiki ijayo baada ya kukamilika kwa taratibu mbalimbali.

 

“Kwa kifupi niwaahidi mashabiki wa Yanga kuifanyia makubwa katika msimu ujao, nimepata taarifa za kuukosa ubingwa kwa misimu miwili mfululizo.

 

“Kwa kuanza nitaanza na ubingwa kwanza na baadaye kulipa kisasi cha msimu uliopita kuwafunga wapinzani wetu wakubwa Simba,” alisema Bigirimana.

 

Comments are closed.