The House of Favourite Newspapers

MAKONDA AFANIKISHA SAFARI NA MATIBABU YA AHMED ALBAITY CHINA


NDOTO na shauku ya kijana Ahmed Albaity alieteseka kwa zaidi ya Miaka 10 Kitandani kwa kushindwa kumudu gharama za matibabu leo imebadilika kuwa furaha baada ya Mkuu wa Mkoa wa Dar es salaam Mhe. Paul Makonda kumkabidhi Tiketi za Ndege za watu Wanne kwaajili ya safari ya kwenda kupatiwa matibabu Nchini China kwenye Hospital ya Beijing Puhua International huku akijitolea pia kugharamia fedha za Matibabu na Malazi.

 

RC Makonda alitoa ahadi kumsaidia Ahmed Albaity wakati wa Zoezi la Upimaji Afya Bure kwenye Meli ya Jeshi la China mwishoni mwa Mwaka Jana baada ya kugundulika Ahmed anahitaji Matibabu Maalum ambayo hayapatikani kokote kule duniani isipokuwa China, jambo lililomfanya RC Makonda kutokwa na Machozi na Kuhaidi Kumpeleka kwenye matibabu kwa gharama yoyote ile Maumivu na Mateso anayopitia kijana huyo.

 

Ahmed Albaity anasumbuliwa na tatizo la uti wa mgongo baada ya kuanguka na kuvunjika Shingo alipokuwa akiogelea ambapo kwa sindano moja pekee inagharimu Dollars 26,000/= sawa na shillingi million 52.

 

RC Makonda amesema Ahmed atasafiri Nchini China Siku ya Jumapili akiongozana na watu watatu wa kumsaidia kumuhudumia ambapo gharama zake ni zaidi ya Shilingi Million 100.

 

Aidha RC Makonda amesema Shauku yake ni kugusa maisha ya Mwananchi hata kama ni mmoja atakaekwenda mbele za Mungu na kusema Asante Mungu kwa kutupatia viongozi wetu, ifike mahali tumtumikie Mungu katika nafasi zetu, na katika hilo watu wote watakuwa Sawa na tutawahudumia bila kutarajia chochote kutoka kwao kama sehemu ya utumishi wetu ambapo amewashukuru watu wote waliomchangia na kufanikisha matibabu.

 

 

Hata hivyo RC Makonda ametoa wito kwa wananchi wa dini zote kumuombea Ahmed ili aweze kupona na kuendelea na shughuli za ujenzi wa Taifa.

 

Kwa upande wa Ahmed Albaity amemshukuru RC Makonda kwa moyo wa ukarimu aliouonyesha ambapo ameeleza kuwa ameishi kwa mateso muda mrefu kutokana na kukosa uwezo wa kumudu gharama za matibabu.

 Aidha amesema alipokuwa akiomba watu wamchangie wapo waliokuwa wakimvunja moyo kwa kumwambia hawezi kupona lakini RC Makonda ameonyesha moyo wa kipekee.

Comments are closed.