The House of Favourite Newspapers

Video: Maswali 7 Tata Kumhusu Scorpion

uwazi-1

UWAZI MA: DAR ES S A L A A M : Tukio la ukatili wa kupindukia a l iot endewa kijana Said Mrisho la kuvamiwa, kuchomwa visu na bisibisi, kutobolewa macho na kuporwa fedha, bado linaendelea kusumbua vichwa vya wengi huku mtuhumiwa Salum Njewele ‘Scorpion’ (34) aliyepandishwa kizimbani kwa mara ya pili Jumatano iliyopita, akiibua maswali saba (7) tata kumhusu, Uwazi limechimba.

SCORPION CHINI YA ULINZI: Mtuhumiwa wa unyang'anyi wa kutumia silaha, Salum Njwete maarufu 'Scorpion' akisindikizwa chini ya ulinzi wa polisi na askari magereza kuelekea kwenye basi la magereza kurudishwa rumande huku akicheka baada ya waandishi kubaini mbinu zake za kubadilisha nguo ili wasimtambue baada ya kusomewa shitaka lake katika Mahakama ya Wilaya ya Ilala, Dar es Salaam jana. Mtuhumiwa huyo anadaiwa kumvamia na kumtoboa macho mkazi mmoja wa Dar es Salaam hivi karibuni. (Na Mpigapicha Wetu).Mtuhumiwa Salum Henjewele ‘Scorpion’.

Tangu kutokea kwa tukio hilo, timu ya waandishi makini wa gazeti hili, imekuwa mtaani ikijikita eneo tajwa la Buguruni, Dar, kuchimba kwa kina kuhusu tukio hilo na mtuhumiwa wake, Scorpion na yafuatayo ni maswali saba tata yaliyoibuka yakimhusu jamaa huyo.

NDUGU, MARAFIKI WANALIJUA JINA LA SCORPION?
Jina la Scorpion lilianza kuvuma tangu siku ya tukio, watu mbalimbali wakimtaja kwamba ndiye mtuhumiwa wa ukatili huo na kwamba alikuwa maarufu mitaa yote ya Buguruni lilikotokea tukio hilo.
Hati ya mashtaka aliyosomewa mtuhumiwa huyo, ikamtaja kwamba jina lake ni Salum Njewele tu bila ya la umaarufu wake. Hata hivyo, uchunguzi uliofanywa na gazeti hili ukiwahusisha watu wake wa karibu sana, akiwemo nduguye, unaonesha kwamba Scorpion ni jina analolitumia zaidi kwenye michezo yake ya ngumi (karate).

KWA NINI ALICHAGUA JINA LA SCORPION?
“Alilichagua jina hilo kwa sababu watu wengi wa karate wanapenda kujiita majina kama hayo. Mfano mimi mwalimu wake najiita Dragon. Kuna mwingine ambaye ni baunsa wa kiongozi mmoja wa chama cha siasa nchini…(anamtaja jina) yeye anajiita Cobra. Kifupi ni kwamba, wacheza karate wengi duniani wana majina nje ya kwao ya asili na wengi hupenda kutumia majina ya wanyama au wadudu,” alisema mwalimu wa karate wa Scorpion al iyej i tambul i sha kwa jina la Kaizile Jabiry.

ANA A.K.A NYINGINE?
Kuhusu hilo, muandaaji wa sinema za Bongo, Tuesday Kihangala ‘Mr. Chuz’ alisema:
“Mbali na Scorpion, mimi nalijua jina la Samjet. Hili jina alilitumia zaidi kwenye mazoezi yake ya karate kwani alipenda kuruka juu kama ndege f’lani hivi. Si unajua tena.”

NI KWELI ALIKUWA BAUNSA WA KIMBOKA?
Kimboka ni baa maarufu iliyopo eneo la Buguruni- Sheli. Muda mfupi baada ya kutokea kwa tukio hilo, yalisambaa madai mitaani kwamba, Scorpion alikuwa mlinzi (baunsa) katika baa hiyo na alikuwa akitumainiwa kwa kuwadhibiti vibaka na wahalifu katika eneo hilo.
Hata hivyo, akiongea na Uwazi mwishoni mwa wiki iliyopita, mfanyakazi mmoja wa baa hiyo aliyejitambulisha kwa jina moja la Manka, alisema hamjui Scorpion.

NI MKAZI WA WAPI?
Muda mfupi baada ya tukio la Scorpion kudaiwa kumjeruhi Said na kumtoboa macho, watu mbalimbali waliohojiwa, walidai kwamba, mtuhumiwa huyo ni mkazi wa Buguruni- Kwamnyamani na kwamba ni maarufu maeneo hayo na kuwa, hakuna mtu ambaye hamjui.
“Kiukweli hata hafahamiki makazi yake halisi ni wapi ila hakai Buguruni, Yombo wala Tabata, hata watu wake wa karibu ukiwauliza, hakuna anayejua anaishi wapi,” kilisema chanzo chetu, maelezo ambayo yalipewa nguvu na mwalimu wake, Kaizile ambaye alisema licha ya kuwa naye karibu kwa kipindi kirefu, hakujua anakoishi.
Baadaye, baadhi ya vyombo vya habari vikaripoti kwamba Scorpion ni mkazi wa Yombo na vingine vikisema ni mkazi wa Tabata.
Lakini kwa mujibu wa taarifa za kimahakama, mtuhumiwa huyo ni mkazi wa Buguruni- Machimbo jijini Dar es Salaam hivyo umaarufu wake maeneo ya Buguruni uko wazi.

JE, NI TUKIO LA KISASI?
Katika tukio hilo, baadhi ya watu waliozungumza na Uwazi walidai ukatili aliofanyiwa Said si wa kawaida na kwamba, kuna kitu kinafichika nyuma ya pazia huku wengine wakidai kuna dalili za kisasi.
Pia ACP Salum alilifafanua hilo: “Kwa kweli mimi sijaweza kuthibitisha motive (sababu au kisa) hasa kuwa ni nini. Lakini mimi naona ni uhalifu wa kawaida tu.”

AMEOA, HAJAOA?
Miongoni mwa maswali tata kuhusu mtuhumiwa huyo, lilikuwa ni kama ameoa au anaishi mwenyewe ambapo kila mtu alikuwa akizungumza lake. Lakini baada ya uchunguzi wa Uwazi, imebainika kwamba, Scorpion amewahi kuoa lakini baadaye akaachana na mkewe. Kwa hiyo mpaka tukio hilo linatokea, alikuwa akiishi mwenyewe.
Maelezo hayo yalipewa nguvu na Mr Chuz aliyethibitisha kwamba Scorpion amewahi kuoa lakini ‘akazinguana’ na mkewe, wakaachana.

WACHUNGAJI WAMUITA MAJERUHI MAKANISANI
Wakati huohuo, kuna habari kwamba, baadhi ya wachungaji wa makanisa ya kiroho nchini, wamemuita kijana aliyetobolewa macho, Said kuhudhuria ibada kwenye makanisa ili kumwombea apone na kuweza kuona tena licha ya madaktari wa Hospitali ya Taifa, Muhimbili kusema hawezi kuona tena!
“Unajua kidaktari ni sawa kabisa, hawezi kuona tena maana ameondolewa hadi goroli. Lakini kwa Mungu goroli zinaweza kurudi kwani yeye si ndiyo muumbaji bwana! Nini kwake kinashindikana?” alisema mchungaji mmoja wa kanisa la kiroho lililopo Temeke aliyejitambulisha kwa jina moja la Mathayo.

MAMA RWAKATARE: ANAWEZA KUONA TENA ENDAPO…
Naye Mchungaji Kiongozi wa Kanisa la Mlima wa Moto Assemblies of God, Mikocheni B, mama Getrude Rwakatare alipoulizwa kuhusu wachungaji kumuita majeruhi huyo ili kumwombea, alisema:
“Mimi siyo Mungu na wala si mponyaji. Kama anakuja kanisani nikatoa neno mimi au akaenda makanisa mengine kwa imani yake kwamba Mungu anaweza kumponya, anaweza kuona tena! Lakini iwe kwa imani yake na si kwa kujaribu.


“Kwa hiyo hata akija kwangu kwa imani, nitamwombea kwa Mungu kwani yeye ndiye anayeponya wanadamu wenye matatizo mbalimbali lakini si mimi kama nilivyo.”
Kauli ya mama Rwakatare inaongezewa nguvu zaidi na mchungaji mwingine wa Kanisa la Bwana lenye makao yake, Ilala, Dar, Ezekiel Mhaga ambaye alisema kuwa Said kuona tena si suala la kutilia shaka endapo mwenyewe atakuwa na imani.
“Kwani Said ni nani hata Mungu asimtendee muujiza wake wa kuona tena? Tena basi, Mungu anapenda kujiinua pale ambapo, uwezo wa binadamu na utaalam wa elimu umeshindwa,” alisema mchungaji huyo.

YAMEKUJAJE HAYA?
Kauli za watumishi hao wa Mungu, zimekuja kufuatia majibu ya madaktari wa Hospitali ya Muhimbili ambapo Said alipelekwa na Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda kusema uchunguzi wao umebaini kuwa majeruhi huyo hawezi kuona tena, hali iliyoibua vilio kwa mhusika na mkewe.
Imeandikwa na Hashim Aziz, Gabriel Ng’osha, Leonard Msigwa na Sifael Paul.

Comments are closed.