Mawazo kuagwa leo jijini Mwanza, kuzikwa kesho Geita
Mkutano wa kutoa ratiba za kuuaga mwili wa Marehemu Mawazo kwa wanahabari Jijini Mwanza jana.
Mwili wa aliekuwa Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo Chadema Mkoa wa Geita Marehemu Alphonce Mawazo, leo unatarajiwa kuagwa katika Viwanja vya Furahisha Jijini Mwanza kabla ya kusafirisha kwenda Mkoani Geita humo kwa ajili ya Mazishi.
Kaimu Katibu Mkuu wa Chadema Salum Mwalimu, alisema Marehemu Mawazo ataagwa Kitaifa kwa taratibu za chama hicho, katika uwanja wa Furahisha Jijini Mwanza.
Alisema ratiba hiyo itatanguliwa na ratiba ya kifamilia ya kuuaga mwili huo, ambayo itafanyika asubuhi Nyegezi Jijini Mwanza ambako ni nyumbani kwa Mchungaji Charles Lugiko ambae ni baba mdogo wa Marehemu Mawazo hiyo ikiwa ni baada ya mwili wake kutolewa katika Hospitali ya Rufaa Bugando ulikohifadhiwa.
Mwalimu amebainisha kwamba mwili huo utasafirishwa kwenda Mkoani Geita kuanzia majira ya saa nane mchana ambapo wakazi wa Mkoa huo pia watapata fursa ya kuuaga kesho kutwa jumapili.
Allieleza kwamba kuanzia majira ya saa mbili asubuhi, shughuli za kuuaga mwili huo zitafanyika Kimkoa katika Uwanja wa Magereza Mjini Geita na baadae kusafirisha kwenda Katoro ambapo wakazi wa Jimbo lake la Busanda watapata fursa ya kuuaga mwili huo.
Mwalimu aliongeza kuwa, baada ya shughuli zote hizo kukamilika, mazishi ya Marehemu Mawazo yanatarajiwa kufanyika siku ya Jumatatu katika Kijiji cha Chikobe Jimbo la Busanda Mkoani Geita.
Shughuli zote hizo zinatarajiwa kuongozwa na Mwenyekiti wa Chadema Taifa Freeman Mbowe, Viongozi waandamizi wa Chama hicho akiwemo Frederick Sumaye, aliekuwa mgombea urais wa Ukawa Edward Lowasa, wabunge pamoja na makada wa Chadema.
Ratiba za Mazishi ya Marehemu Mawazo ambae aliuawa Novemba 14 mwaka huu na watu wasiojulikana, zimejiri baada ya Mahakama Kuu Kanda ya Mwanza jana kuondoa zuio la Jeshi la Polisi Mkoani Mwanza, lililokuwa zinazuia mwili huo kuagwa Jijini Mwanza kutokana na hofu ya kiusalama pamoja na uwepo wa mlipuko wa ugonjwa wa kipindupindu ambapo zuio hilo liliondolewa katika kesi
iliyofunguliwa na baba mlezi wa Mawazo, Mchungaji Charles Lugiko baada mvutano mkali wa siku nne mahakamani hapo.
Comments are closed.