KITENDO cha Kagera Sugar kuwa na matokeo mabaya msimu huu, kimetajwa kuwa ni kukosekana kwa mfungaji mahiri ndani ya kikosi hicho kama alivyokuwa Mbaraka Yusuf ambaye kwa sasa anaitumikia Azam FC.
Mbaraka kabla ya kuihama timu hiyo, msimu uliopita aliisaidia kufanya vizuri ambapo alifunga mabao 12 huku timu hiyo ikimaliza nafasi ya tatu ikiwa na pointi 53.
Kabla ya mechi za jana Jumapili, Kagera Sugar ilikuwa nafasi ya 14 ikiwa na pointi 18, ikiwa imefunga mabao 12 pekee ambayo msimu uliopita yalifungwa na Mbaraka peke yake. Kwa sasa Venus Ludovick ndiye kinara wao akiwa na mabao matatu akifuatiwa na Jafar Kibaya na Edward Christopher ambao kila mmoja ana mabao mawili.
Akizungumzia hilo, Maxime alisema: “Timu zetu hizi ndogo tunakuwa na changamoto nyingi sana hasa katika kuwaandaa wachezaji ambao watakuja kukusaidia, msimu uliopita tulikuwa na Mbaraka ambaye alikuwa analijua haswa goli, msimu huu hayupo kikosini kwetu.
“Sasa tunaendelea kumuandaa mchezaji mwingine ili aweze kuwa kama yeye jambo ambalo ni nadra sana kulifanikisha kwa kiwango kile ukitakacho kwa sababu wachezaji wanatofautiana.
“Wenzetu timu hizi kubwa zina kila kitu na zina uwezo wa kumchukua mchezaji yeyote wanayemtaka, kwetu ni changamoto, lakini tutaendelea kupambana, mechi bado zipo nyingi naamini tutafanya vizuri.”
Omary Mdose, Dar es Salaam
Comments are closed.