The House of Favourite Newspapers

MICO Halal Tanzania Yapata Cheti cha Kimataifa Cha Ithibati

0
Mwakilishi wa Mufti wa Tanzania ambaye ni Katibu wake, Musa Bin Hemed akizungumza kwenye hafla ambayo Kampuni ya MICO International Halal Bureau of Certification (MIHB), ilipewa cheti cha kimataifa cha kutoa ithibati ya Halal ya kimataifa kwa bidhaa mbalimbali ikiwemo nyama.

KAMPUNI ya MICO International Halal Bureau of Certification (MIHB), imefanikiwa kupata cheti cha kimataifa kitakachoiwezesha kutoa ithibati ya Halal ya kimataifa kwa bidhaa mbalimbali ikiwemo nyama inayotumika nchini na inayosafirishwa kuuzwa nje ya nchi.

 

Kwa kupata cheti hicho kwa mara ya kwanza sasa Tanzania imepata kampuni iliyokidhi vigezo vya kimataifa vya ithibati ya Halal (MIHB) ambaye ni wakala wa Baraza Kuu la Waislamu Tanzania (Bakwata).

 

Hafla ya kukabidhi cheti hicho imefanyika Dar es Salaam na kuhudhuriwa na Mwakilishi wa Mufti wa Tanzania ambaye ni Katibu wake, Musa Bin Hemed na wawakilishi wa taasisi ya Uturuki iliyotoa cheti hicho ya Hafsa Halal Murat Bayka na Jalal Sahal.

Mkurugenzi Mkuu wa Kampuni ya MICO International Halal Bureau of Certification (MIHB), kushoto, Hassan Mchomvu akipokea cheti cha kimataifa cha kutoa ithibati ya Halal ya kimataifa kwa bidhaa mbalimbali ikiwemo nyama kutoka kwa ofisa wa Hafsa ya Uturuki Murat Bayka. Kulia ni Mwenyekiti wa Wanawake Waislamu Tanzania, Shamim Khan na kushoto ni Mweka Hazina wa Baraza Kuu la Waislamu (BAKWATA), Sheikh Said Mwenda.

Akizungumza kwenye hafla hiyo, Sheikh Mwenda Said ambaye ni Mweka Hazina Mkuu wa Baraza Kuu la Waislamu (Bakwata), alisema cheti hicho kimetolewa baada ya Bakwata kupitia mdau wake MICO International Halal Bureau Limited kuendesha mafunzo ya kuwaongezea wataalamu wao uwezo.

 

Alisema Hafsa Halal Certification and Food Import and Export Limited ya Uturuki kwa kushirikiana na MICO walianza kuwaongezea ujuzi watu hao kwa njia ya zoom kuanzia mwezi wa tatu mwaka huu na kuja kukamilisha mafunzo hayo ya ana kwa ana kuanzia Julai Mosi hadi sasa ambapo wamefikia viwango vinavyotakiwa kimataifa.

 

Alisema wakufunzi hao wataendelea kutoa elimu ya Halal katika kila Mkoa Tanzania Bara na kwa ikilazimu pia wataenda Visiwani Zanzibar na kwamba MICO Halal imepata uwezo wa kutoa huduma za  ithibati ya Halal kama nyama na bidhaa mbalimbali ndani ya nchi na kimataifa.

Mwakilishi wa Kampuni ya Hafsa Halal Certification and Food Import and Export Limited ya Uturuki, Murat Bayka akizungumza kwenye hafla hiyo ambapo MICO International Halal Bureau of Certification (MIHB), ilipewa cheti cha kimataifa cha kutoa ithibati ya Halal ya kimataifa kwa bidhaa mbalimbali ikiwemo nyama.

Akizungumzia umuhimu wa kuwa na cheti cha kimtaifa cha Halal, Sheikh Mwenda alisema bidhaa za Tanzania zitakubalika katika soko la kimataifa hasa nyama na kuongeza pato la taifa litakalosaidia kukuza uchumi na kuongeza wigo wa ajira.

 

Alitaja faida nyingine kuwa ni bidhaa za Tanzania hususan nyama kukubalia kwenye soko la kimataifa kama uarabuni na barani Asia ambako huwa hawakubali bidhaa ambayo haina nembo ya Halal.

 

Alisema cheti hicho kitasaidia kuipatia nchi fedha za kigeni kwani kampuni za ndani zitakuwa na uwezo wa kusafirisha bidhaa mbalimbali ikiwemo nyama kwenye mataifa mbalimbali duniani.

Wanawake waliopata mafunzo ya kimataifa kuhusu bidhaa za Halal wakiwa kwenye picha ya pamoja na viongozi wa Kampuni ya MICO International Halal Bureau of Certification (MIHB), ilipewa cheti cha kimataifa cha kutoa ithibati ya Halal ya kimataifa kwa bidhaa mbalimbali ikiwemo nyama pamoja na viongozi wa Baraza Kuu la Waislamu BAKWATA na Taasisi ya Hafsa ya Uturuki ambayo ilitoa cheti hicho.

“Nchi ilikuwa inapata hasara kwasababu makampuni ya ndani yalikuwa yanachukua ithibati ya Halal nje ya nchi kama Australia, Quatar na kwingineko lakini sasa MICO Halal Tanzania itafanyakazi hiyo na fedha zitabaki hapa nchini,” alisema

 

 

Alisema ili kuboresha huduma za Halal, Bakwata na mdau wake MICO Halal International wanaomba serikali iwawezeshe kupata maabara ya Halal kupitia wadau mbalimbali ili kutoa huduma stahili.

 

Alisema wanaiomba serikali isaidia kuwaambia wafanyabiashara wanaenda kupata ithibati ya Halal nje ya nchi kama Afrika Kusini, Australia na kwingineko kuwa BAKWATA kupitia wakala wake MICO sasa wanatoa hiyo ithibati hapahapa nchini.

Leave A Reply