The House of Favourite Newspapers

Msuva: Chongeni Tu, Ila Yanga Bingwa

Saimon Msuva.

STRAIKA wa Difaa Al Jadida ya Morocco na Taifa Stars, Saimon Msuva, amesema kwa namna alivyoishuhudia Yanga katika Kombe la Mapinduzi, itakuwa ngumu kufungika katika Ligi Kuu Bara kwani vijana waliopewa nafasi wameshajiamini na wataipa ubingwa.

 

Msuva ambaye msimu uliyopita aliisaidia Yanga kutwaa ubingwa wa ligi kuu kwa mara ya tatu mfululizo, hivi karibuni alirejea nchini kutoka Morocco kwa mapumziko mafupi.

Kikosi cha timu ya Yanga.

Hadi sasa akiichezea Difaa, Msuva ameifungia timu hiyo mabao matano kwenye michezo 14 ya Ligi Kuu ya Morocco.

Akizungumza na Championi Jumamosi alisema vijana hao akiwemo Yohana Nkomola, Ramadhan Kabwili na Said Musa wameweza kufanya vizuri hivyo wataiwezesha Yanga kutwaa ubingwa bila kufungwa katika michezo iliyosalia.

 

“Kwa jinsi nilivyoifuatilia Yanga katika Kombe la Mapinduzi, hakuna mwaka ambao imeweza kutumia vijana wengi kama mwaka huu katika michuano hiyo na wamefanya vizuri.

 

“Yanga imeandaa watu wengi wa kupambana kiasi kwamba kikosi chao kimepata wachezaji wengi sana na kukifanya kuwa kipana, kwa kasi yao ile ya Mapinduzi nina imani hata ligi kuu wataisaidia sana hawa vijana.

 

“Wale vijana kila mmoja ameshajiamini na ana machungu ya kuchukua kombe hivyo wapinzani wao wajipange sana kwani uwezekano wa kutetea ubingwa wao umeongezeka na kuwa mkubwa,” alisema Msuva.

 

Katika Kombe la Mapinduzi, Yanga iliishia katika nusu fainali ilikotolewa na URA ya Uganda kwa penalti 5-4, wiki ijayo inacheza na Mwadui FC mechi ya ligi kuu.

Comments are closed.