The House of Favourite Newspapers

MTOTO MIAKA 5 KUONDOLEWA KIZAZI!

DAR ES SALAAM: EE Mungu! Ndiyo kauli unayoweza kuiotoa kumuonea huruma mtoto wa miaka 5 ambaye madaktari wamemtaka afanyiwe upasuaji wa kumuondoa kizazi ili kunusuru maisha yake.

 

Mtoto huyo aishiye mkoani Dodoma ambaye jina lake tunalihifadhi, aliripotiwa na gazeti hili hivi karibuni akisumbuliwa na tatizo la kupata hedhi akiwa na umri huo mdogo.

 

Baada ya kuzidiwa hivi karibuni, mwishoni mwa wiki iliyopita alihamishiwa katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili jijini Dar kwa ajili ya matibabu zaidi. Akizungumza na Ijumaa Wikienda wakati akiwa Muhimbili, mama mzazi wa mtoto huyo Loveness Samwa alisema kwamba kadiri siku zinavyozidi kwenda ndivyo hali ya mwanaye inavyozidi kuwa mbaya.

 

“Nakumbuka ilikuwa tarehe 13, mwezi huu mwanangu aliingia tena siku zake akawa anajisikia maumivu, nikajua labda ni kawaida tu lakini ilipofika kesho yake ndio hali yake ikazidi kuwa mbaya.

“Tumbo likawa linamuuma sana mpaka akapoteza fahamu. Alivyopoteza fahamu nilichanganyikiwa sana ikabidi nimpeleke tena Hospitali ya General Dodoma, nashukuru Mungu madaktari walimpokea vizuri na wakamwekea Oxygen ili iweze kumsaidia kupumua,” alisema kwa masikitiko mzazi huyo.

 

Akizidi kuelezea tatizo hilo la mwanaye, mama huyo alisema siku hiyo ilipita bila mwanaye kuamka, daktari akamwambia kuwa, mwanaye ana tatizo kubwa ambalo wao hawalimudu. “Wakaniambia ninatakiwa nije Muhimbili kwa hiyo nichangie shilingi laki 1 ya Ambulance. “Nilimwambia daktari kwamba sina hiyo hela, alinielewa akaandika barua ikapelekwa kwa mkurugenzi na nashukuru pia yule mkurugenzi alinielewa hivyo ukafanyika utaratibu wa mimi kuja Muhimbili.

“Tulifika hapa Muhimbili saa 4 asubuhi, madaktari walivyotuona wakaanza kumtibia kwanza mwanangu kwa sababu alikuwa bado hajapata fahamu, walimchukua na kuanza kumfanyia vipimo ambapo wakati nasubiria majibu walimtundikia maji wakamuwekea na Oxygen ambapo alikuja kuzinduka saa 11 jioni.

 

“Daktari aliniita tena kwa ajili ya kunipa majibu ambapo aliniambia kwamba kipindi mtoto wangu anapata siku zake, kuna damu ilienda kuganda kwenye kizazi, hivyo kusababisha kiharibike, kwa hiyo anatakiwa afanyiwe upasuaji ili kuondoa kizazi kwa lengo la kuokoa maisha yake.

 

“Daktari ameniambia, atakapoondolewa kizazi ataacha kublidi, lakini natakiwa niwe na shilingi 1, 400,000 ili Jumatatu (leo) mwanagu afanyiwe oparesheni na mimi hapa nilipo sina hela kabisa kwa sababu nilichangiwa kama shilingi 200,000 hivi ambayo nayo nimeimaliza kwenye vipimo, naomba Watanzania wandelee kunisaidia ili niokoe maisha ya binti yangu kwa sababu bila hiyo pesa mwanangu hataweza kufanyiwa oparesheni.

 

“Mungu uwabariki wale wanaojitoa na kusaidia wenzao wenye matatizo kwa moyo wao wote,” alisema mama huyo. Mbali na kukabiliwa na changamoto ya ugonjwa wa mwanaye, mama huyu hana mume wala ndugu wenye uwezo, kula na kulala kwake ni kwa shida hivyo kwa yeyote aliyeguswa anaweza kumsaidia chochote alicho nacho kwa namba zake ambazo ni 0764361804.

Stori: Memorise Richard,Ijumaa Wikienda

EXCLUSIVE: ‘BABA D’ ANAONGEA NA DIAMOND AFANYE NAE KOLABO |+255 GLOBAL RADIO

Comments are closed.