Muumini Azindua Bendi Mpya Aja na Fenesi, Sitaki Kuhamia Kwa Mparange
MKONGWE wa dansi nchini, Mwinjuma Muumini ambaye amewahi kumiliki bendi kadhaa ambapo mwaka jana alizindua bendi yake ya Shadai ambayo ilidumu kwa miezi kadhaa na kusambaratika leo amezindua tena bendi yake nyingine iitwayo Special Band ‘Wana Tamtam’.
Muumini amefanya uzinduzi huo kwenye mkutano na wanahabari uliofanyika Ufukwe wa Coco, Dar na kuzitaja nyimbo nne walizokuja nazo ukiwemo Fenesi, Kwa Mparange Sihami, Vumbi la Congo na nyinginezo.
Katika nyimbo hizo Mwinjuma aliuelezea utamu wa fenesi na karaha zake ambapo maswali mengi yaliibuka baada ya kuutambulisha wimbo wake mpya ujao uitwao Sihami kwa Mparange wengi wakitaka kujua maana yake.
Katika bendi Mwinjuma kama kawaida yake yuko na wakongwe wenzake, Rashidi Sumuni, Salma Mjukuu na wengineo.
Pamoja na wakongwe hao Mwinjuma amewetangaza wanamuziki chipukizi kadhaa aliosema amechanganya damu hiyo changa kwenye bendi yake ili kuleta mapinduzi kwenye burudani ya kizazi kipya.
Katika mkutano huo Mwinjuma amesema bendi hiyo imekuja na baraka baada ya kupata shoo za nje ya nchini siku chache kabla ya uzinduzi wa leo.
HABARI/PICHA: RICHARD BUKOS /GPL