The House of Favourite Newspapers

Mwakyembe: Kuanzia Mei Mosi… Marufuku Kufunga Ndoa Bila Cheti cha Kuzaliwa

Waziri wa Katiba na Sheria, Dkt. Harrison Mwakyembe amesema kuwa kuanzia, Mei Mosi mwaka huu ni marufuku watu kufunga ndoa ya aina yoyote, iwe ya serikali, ya dini au ya kimila bila kuwa na cheti cha kuzaliwa.

Waziri Mwakyembe amesema hayo leo akiwa katika ziara yake mkoani Morogoro.  Ameongeza kuwa serikali imeamua kufanya hivyo ili kupata takwimu sahihi za wananchi wake zitakazosaidia kupanga mipango ya kimaendeleo sambamba na kuzuia wageni kuingia nchini bila kufuata utaratibu uliowekwa.

Pia, Dkt. Mwakyembe amewataka Wakala wa Usajili, Ufilisi na Udhamini (RITA), kuhakikisha inasimamia sheria ya usajili ambapo amesema kuwa kutokuwepo kwa takwimu sahihi za vizazi na vifo ama ndoa husababisha nchi kushindwa kusonga mbele kimaendeleo.

“Wenzetu wa nchi zilizoendelea suala la usajili wamelipa kipaumbele lakini sisi bado tuko nyuma, kwa mfano Mkoa wa Morogoro kwa mujibu wa sensa ya watu na makazi ya mwaka 2012, inaonyesha kuna jumla ya wakazi milioni 2.2, lakini waliosajiliwa na kuwa na vyeti vya kuzaliwa ni asilimia 11 pekee huku wengine wakiwa bado hawasajiliwa,” amesema.

Comments are closed.