The House of Favourite Newspapers

Mwanzilishi wa Tukuyu Stars Kuzikwa kwa Kuchomwa Moto – Picha

MAMIA ya waombolezaji wamejitokeza kuuaga mwili wa marehemu Ramnik Patel ‘Kaka’, ambaye alifariki Oktoba 18 mwaka huu, nyumbani kwao Uhindini mkoani Mbeya ambapo kulingana na taratibu na mila za Kihindu, mwili wa mwanzilishi huyo wa timu ya soka ya Tukuyu Stars utazikwa kwenye makaburi ya Sabasaba jijini Mbeya kwa kuchomwa moto.

Patel alifariki dunia baada ya kusumbuliwa na maradhi ya mguu kwa muda mrefu kutokana na kuvunjika mfupa wa nyonga kwenye mguu wake wa kushoto na kulazwa katika Hospitali ya Rufaa ya Jiji la Mbeya tangu Agosti mwaka huu kwa ajili ya kupatiwa matibabu.  Hata hivyo, aliruhusiwa baada ya afya yake kuimarika na kuendelea kuugua akiwa nyumbani.

Patel maarufu kwa jina la Kaka au Banyambala ambaye diye mwanzilishi wa timu hiyo, atakumbukwa kwa kuipandisha daraja na kuiewezesha Tukuyu Stars kutwaa Ubingwa wa Ligi Kuu Tanzania Bara mwaka 1986, pamoja na kuwaibua wachezaji kadhaa nyota waliotamba nchini.

 

Hata hivyo, msimu wa 1987 iliteremka daraja na Kaka akahangaika nayo hadi kuipandisha tena msimu wa 1988 alipoirejesha Ligi Kuu na kuikabidhi kwa Halmshauri ya Wilaya ya Tukuyu, ambako huko ndipo ilidhoofika.

 

 

Tukuyu inakumbukwa kwa kuibua vipaji vya nyota wengi wa soka mara zote, kuanzia akina Salum Kabunda ‘Ninja’, Justin Mtekere (wote marehemu), Godwin Aswile ‘Scania’ na baadaye akina Stephen Mussa (sasa marehemu) na Sekilojo Chambua.

Aliyewahi kuwa kocha wa timu hiyo, mwaka 2001 hadi 2004, Chuma Amos, alisema watamkumbuka marehemu hasa katika mchango wake wa kuhamasisha mchezo katika Mkoa wa Mbeya.

 

“Tukuyu Stars ndiyo ilikuwa timu ya kwanza Mkoa wa Mbeya kushiriki ligi kuu na kutwaa ubingwa, na baadaye kukapelekea kuibuka kwa timu nyingine kama Mecco, 44 KJ, pamoja na Tiger ambayo ilikuwa ya Tunduma,” alisema Amos.

Marehemu ameacha wajane wawili na watoto watatu. Mwenyezi Mungu ailaze mahali pema peponi, AMEN!

RC AGGREY MWANRI “Nacheza hadi nakalia mpira, kama Gattuso vile”

Comments are closed.