The House of Favourite Newspapers

Nay wa Mitego Tuoneshe Msela Asiyependa Maisha Mazuri

0

EMMANUEL Elibariki ndilo jina lake halisi, lakini kwa mashabiki wa Bongo Hip Hop, wao wanamfahamu zaidi kama Nay wa Mitego, rapa mmoja hivi mgumu, mtoto wa mjini na mwingi wa maneno ya shombo juu ya wenzake katika nyimbo zake.

Nimesema mara nyingi na wala sioni vibaya kurudia tena, kwamba mimi ni shabiki mkubwa wa huyu jamaa. Kinachonifanya nimkubali, ni ule ujasiri wake wa kusema anachokiamini, ingawa mara nyingi kinamletea matatizo kwa namna ya uwasilishaji wake, yaani lugha anayoitumia.

Mimi napenda kuamini katika vile ilivyo, yaani kama mtu anajipendekeza, naamini hivyo, kama ni jasiri, ni mwongo, mnafiki, bendera fuata upepo na vitu kama hivyo. Ni bora ninyamaze kuliko kuita makande kuwa ubwabwa, hata kama yatawekewa maziwa. Nay ni mwimbaji jasiri, asiyeogopa kuzungumza katika hisia zake na amefanya hivyo mara nyingi kupitia tungo zake.

Baadhi zimempa matatizo, zingine zikimpatia maadui na wakati mwingine hata kupunguza ‘funbase’ yake, kitu ambacho katika muziki au shughuli yoyote ni jambo la kawaida kwa sababu uzoefu unatuambia hata mitume walikuwa na maadui, sembuse binadamu? Msikilize katika nyimbo kama Muziki Gani, Shika Adabu Yako, Saka Hela, Wapo na Makuzi.

 

Ni nyimbo ambazo ukizisikiliza unaona mistari yake kama anatumia lugha kali, isiyofaa, lakini ndiyo hali halisi kwa sababu Wabongo ‘sometimes’ wanastahili kupewa maneno ‘streit’. Wiki iliyopita tulipata habari za Nay, ambaye ni mwenyeji wa Mkoa wa Kilimanjaro, kuwa ni kama anayumba flani hivi kiuchumi kwa sababu, lile lundo la magari yake mazuri, ya bei mbaya, yamepotea na kuwa amebakiwa na moja tu ambalo ndilo analitumia kwa mishemishe zake. Haya, kwa mujibu wa vyanzo vyetu, ni kuwa aliyapiga bei.

 

Tukajaribu pia kumfikia kwa njia ya simu na kumjulisha kuhusu ubuyu huo. Uzuri hakukataa, alikubali kuwa ni kweli ameuza magari yake yote na hata lile moja ambalo sisi tuliambiwa analo, hanalo. Bahati mbaya hakutueleza kwa nini aliuza, lakini siku chache baadaye kupitia ‘midia’ nyingine, akasema aliamua kuyauza kwa sababu yeye ni mtoto ambaye amezaliwa kutoka familia ya kawaida, hivyo vitu kama magari wala hata siyo vitu vya lazima.

 

Kwani ameshapanda sana daladala na bajaj, kwa hiyo haoni vibaya kurejea usafiri huo. Ni kweli asemeyo, kwamba amezaliwa kitaa na maisha yake yamejaa uzoefu huo. Kwa kauli hii, ananifanya nipate ukakasi kidogo kwa sababu siamini kama ndiyo sababu ya yeye kuuza magari yake.

 

Yaani eti ameuza kwa sababu alizaliwa Manzese na hivyo anataka kurejea kama zamani? Hapana. Hata wale waliozaliwa Mpitimbi, Songea kule mbali, achilia wa Manzese kwa sababu wapo mjini, ambao kila siku wanatembea umbali mrefu kwenda shule, shamba na mahospitalini, wakizipata za kuweza kununua gari, hawawezi kuacha eti kisa wamezoea ‘kuchapa lapa’.

 

Kwangu mimi sioni kama mtu kuuza kitu ni kufilisika, kwa sababu ili kusonga mbele zaidi wakati mwingine unapaswa kuanza upya katika ngazi flani. Ni vyema kama angekaa kimya na kusema anazo sababu za msingi za kuuza, kuliko utetezi huo aliosema, kwa vile hali kama hiyo inawatokea watu wengi tu.

 

Anaweza kuwa alikopa kwa matarajio angerejesha kupitia shoo, lakini kama tunavyojua hivi sasa vyuma vimekaza kila kona, yawezekana imebidi ajinusuru kwa namna hiyo. Yawezekana pia ameamua kuwekeza katika eneo lingine zuri zaidi kwa kuingiza badala ya starehe, yote ni katika kutafuta.

 

Sema bro, kama ulikopa na sasa ‘Majembe’ wamepiga hodi, ili utusaidie na sisi tunaopenda kukopakopa tujue tusipokuwa makini kuna hatari, au kama unafungua mradi mpya, utujuze pia ili nasi tuone namna gani tunaweza kukusanya vidogo tulivyo navyo tukawekeza na kuanza hatua nyingine. Lakini siyo kutuletea stori hizo, za kutufanya tuache udadisi kwa sababu eti wewe ni msela. Msela gani hapendi maisha mazuri?

ZA CHEMBE LAZIMA UKAE OJUKU ABRAHAM, +255 719 786 355

Leave A Reply