The House of Favourite Newspapers

NDOA YA KIBA YAACHA VILIO!

DAR ES SALAAM: Wakati mkali wa Bongo Fleva, Ali Saleh Kiba ‘AliKiba’ akitarajiwa kuangusha bonge la sherehe baada ya kufunga ndoa nchini Kenya, ndoa hiyo imedaiwa kuacha vilio vikali kwa wanawake ambao waliwahi kushea kitanda na msanii huyo, Ijumaa lina mchapo kamili.

 

Kiba alitarajiwa kufunga ndoa hiyo jana mjini Mombasa nchini Kenya kisha kufuatiwa na bonge la sherehe mjini humo huku sherehe nyingine bab’kubwa ikitarajiwa kufanyika nchini mwishoni mwa mwezi huu.

 

 

MTU WA KIBA ANENA

Mtu wa karibu na AliKiba, amepenyeza habari kuwa, licha ya kwamba wao wanasherehekea harusi ya mkali huyo anayetamba na Wimbo wa Seduce Me, nyuma yake kuna vilio vingi kutoka kwa wanawake ambao walitembea na Kiba kabla. “Kama unavyojua Kiba alishazaa watoto wanne, wale watoto kila mmoja ana mama yake. Sasa mama zao wanalia maana nao walikuwa wana matarajio ya kuolewa,” alisema mtu huyo wa karibu aliyeomba hifadhi ya jina na kuongeza:

 

BIBI HARUSI NJIA PANDA

“Kimsingi wamemweka kwenye wakati mgumu mke wa Kiba kwani tayari ana taarifa na kidogo inamtia hofu lakini Kiba amemtia moyo kwamba wote ameshamalizana nao na hakuna hata mmoja atakayeweza kurudisha majeshi tena.”

ASHUSHA HOJA ZA MAANA

Akizidi kushibisha hoja zake, mtu huyo wa karibu na Kiba alikumbushia sakata la hivi karibuni lililoibuliwa na mmoja wa wanawake waliozaa na Kiba ambaye aliibua figisu za kumpeleka Kiba Ustawi wa Jamii kwa madai kuwa msanii huyo hamjali mwanaye. Hata hivyo, sakata hilo liliisha kimyakimya kwani ilibainika kuwa Kiba hakuwa akimnyima mahitaji mtoto huyo kwani alikuwa akiishi kwa mama yake Kiba.

 

 

 

NDOA ILIKUWA MAAMUZI MAGUMU

Mtu huyo wa karibu alikwenda mbali zaidi kwa kueleza kuwa, wakati Kiba anafanya maamuzi ya kuoa, alijua fika kwamba kuna watu watalia kwa ajili yake lakini hakuwa na namna zaidi ya kumuoa, Amina Khaleef ambaye wanaelewana.“Walikuwa wanalia kwa mengi maana kama unavyojua, kila mmoja alikuwa na matumaini kwamba ipo siku labda pengine ataolewa lakini matokeo yake mambo yamekuwa tofauti,” alisema.

KINA JOKATE SASA

Kama hiyo haitoshi, mtu huyo alizidi kushusha ubuyu kuwa mbali na wale waliozaa na Kiba, lipo kundi lingine la warembo maarufu ambao Kiba alidaiwa kutembea nao akiwemo mrembo Jokate Mwegelo, Jacqueline Wolper, Elizabeth Michael ‘Lulu’, Sabby Angel pamoja na Mnyarwanda Kate Pyton. “Yani hawa kila mmoja analia na lake. Kuna wengine walikuwa wanatamani tu kumuona Kiba akiwa single maana walikuwa wanaweza kujiiba naye na kumfaidi hata kama wana watu wao.

 

“Lakini kwa Jokate ni zaidi ya kilio maana kiukweli Jokate alikuwa akimpenda sana Kiba. Alikuwa na mapenzi ya dhati tatizo lilikuwa ni upande tu wa wazazi wake. Alikuwa akiendelea kuwa karibu na Kiba lakini kwa kusikia ndoa, atalia zaidi,” alisema mtu huyo.

 

Ijumaa lilijaribu kumvutia waya Jokate ili kumsikia anazungumziaje tukio hilo la Kiba kuoa, mwanaume ambaye alimpenda kwa dhati lakini simu yake iliita bila kupokelewa. Hata alipotumiwa ujumbe mfupi wa maandishi, hakujibu chochote licha ya kuonekana ujumbe umemfikia.

HUYU HAPA SABBY

Kwa upande wake Sabby Angel alipotafutwa na Ijumaa, alisema hana habari na ndoa ya Kiba kwani hata hajui.“Mimi sijui kwanza kama Kiba anaoa. Siwezi sema lolote,” alisema.

 

WOLPER

Alipotafutwa Wolper kupitia simu yake ya mkononi, alisikiliza kwa makini jina la mwandishi na chombo anachotoka kisha alipoanza kuelezwa kuhusu hisia zake juu ya ndoa hiyo ya Kiba, ‘purukuchuu’, akakata simu.

MMOJA AKIRI KUMWAGA MACHOZI

Ijumaa lilizungumza na mmoja wa warembo ambaye alikuwa akibanjuka naye miezi ya hivi karibuni ambapo aliomba asitajwe jina lakini akaeleza hisia zake kwamba ameumizwa na kitendo cha Kiba kumuacha solemba.“Nimeumia.

 

Kama mwanamke unajua na mimi nilikuwa na ndoto zangu na Kiba lakini kwa kuwa ameamua kuoa, acha nikae pembeni,” alisema mrembo huyo.Kiba anatarajia kutua nchini Aprili 29, mwaka huu na kuangusha bonge la sherehe ambalo linatarajiwa kusheheni mastaa wengi wakiwemo viongozi wa serikali.

MENEJA ANENA

Meneja wa Kiba, Aidan Seif akizungumza na Ijumaa juzikati, aliweka ‘plain’ kuwa sherehe ya Kiba inatarajiwa kuhudhuriwa na watu wengi mashuhuri akiwemo, Rais Mstaafu, Jakaya Mrisho Kikwete na mkewe Salma.

 

Alipoulizwa kuhusu vilio vya warembo ambao walikuwa wapenzi wa Kiba, meneja huyo hakutaka kuzungumzia na kuomba watafutwe wahusika akiwemo Kiba mwenyewe.Ijumaa lilimvutia waya Kiba alioko nchini Kenya ambapo hata hivyo simu yake haikupokelewa.  

Stori: Mwandishi Wetu, Ijumaa

 

Comments are closed.