The House of Favourite Newspapers

Niyonzima Arejea Simba Kimyakimya

BAADA ya mvutano mkubwa na waajiri wake, kiungo mchezeshaji Mnyarwan­da, Haruna Niyonzima atarejea uwanjani na kuanza mazoezi ya pamoja na wenzake wakati wowote baada ya kuminya pilau la sikukuu ya leo.

 

Awali, kulikuwepo na sintofahamu ya kiungo huyo anayemudu kucheza namba 8 baada ya kuchelewa kujiunga na kambi ya pamoja ya timu hiyo iliyoweka nchini Uturuki wakijiandaa na msimu mpya wa Ligi Kuu Bara.

Mnyarwanda huyo alijiunga na Simba kwenye msimu uliopita wa ligi akitokea Yanga baada ya mkataba wake kumalizika wa kuichezea timu ambaye anatarajia kukutana na ushindani kutoka kwa viungo wapya Mzambia, Claytous Chama na Hassan Dilunga.

 

Championi Jumatano limepata taarifa za uhakika kutoka ndani ya Kamati ya Utendaji ya timu hiyo kuwa viongozi na kiungo huyo tayari wamefikia muafaka mzuri na kumrejesha kikosini kwa ajili ya kuanza mazoezi.

Katika kikao hicho inaelezwa kuwa wamekubaliana baadhi ya vitu baada ya viongozi kukiri kulikuwa na up­ungufu ikiwemo kwa Niyonzima kuchelewa kujiunga na timu hiyo kabla ya kukubaliana kiungo huyo kurejea mazoezini.

 

“Niyonzima wakati wowote kuanzia kesho (leo) atarejea uwanjani kwa ajili ya kuanza mazoezi ya pamoja na wenzake katika kuele­kea msimu mpya wa ligi.

“Kurejea kwa Niyonzima kutaimarisha kikosi chetu kinachoundwa na wachezaji wengi wenye uwezo na uzoefu mkubwa utakaoleta changamoto ya ushindani wa namba,”alisema mtoa taarifa huyo.

 

Kwa mujibu wa ripoti ya uchunguzi wa Gazeti ndu­gu la Championi Juma­tano ambalo ni Spoti Xtra, iliyochapishwa kwenye toleo la Jumapili iliyopita Niyonzima alikuwa na shida nne na viongozi wake.

Gazeti hilo lilitaja sababu hizo kwamba ni kukiuka makubal­iano kwenye suala la pango, shule ya watoto wake,uhusiano wake na viongozi pamoja na shinikizo la familia yake.

 

 Wilbert Molandi, Dar es Salaam

Comments are closed.