The House of Favourite Newspapers

NIYONZIMA, JUUKO HUKO SIMBA MAMBO NI MOTOO

 KIUNGO mchezeshaji wa Simba, Mnyarwanda, Haruna Niyonzima na beki wa kati Mganda, Juuko Murshid taratibu wameanza kuingizwa kwenye mipango ya Kocha Mkuu wa timu hiyo, Mbelgiji, Patrick Aussems.

 

Hiyo, ikiwa ni siku chache tangu wajiunge katika mazoezi ya timu hiyo na kuanza programu ya kocha huyo aliyemrithi Mfaransa, Pierre Lechantre.

Wachezaji hao, hivi karibuni walirejea kwenye timu hiyo na Mbelgiji kuwapa wiki mbili hadi tatu kwa ajili ya kuwaangalia kabla ya kuwaingiza katika mipango yake kwa ajili ya kuwatumia katika michezo ya Ligi Kuu Bara baada ya kuchelewa kambi ya kabla ya msimu ‘pre season’.

 

Katika mazoezi ya mwisho kuelekea mchezo dhidi ya watani wa jadi, Yanga, Mbelgiji huyo alionekana kuanza kuwatumia wachezaji hao kwa kuwapanga katika kikosi chake cha pili wakiwa pamoja na Said Ndemla, Yusuph Mlipili na Asante Kwasi.

 

Wakati mazoezi hayo yakiendelea, Niyonzima alionekana akimiliki mpira muda mwingi huku akiuchezea mpira na kupiga pasi safi zilizonyooka kwa wachezaji wenzake.

 

Niyonzima akifanya ufundi wake huo, Juuko yeye alionekana akitimiza majukumu yake vizuri ya kupunguza na kuokoa hatari golini kwake huku akipambana na washambuliaji hatari wa timu hiyo Mganda, Emmanuel Okwi na Mnyarwanda, Meddie Kagere.

Wakati mazoezi hayo yakiendelea, kocha huyo alionekana mara kadhaa akimpa maelekezo Niyonzima na Juuko.

 

Wilbert Molandi, Dar es Salaam

Comments are closed.