The House of Favourite Newspapers

Nyie Mna Mghana, Sisi Tuna Mbrazil

0

MASHABIKI wa Simba ambao jana walijitokeza katika Uwanja wa Taifa, Dar, walikuwa na kazi moja tu ya kuwajibu wenzao wa Yanga kuwa ‘Nyie mna Mghana, sisi tuna Mbrazili mabao.’

 

Jeuri hiyo ya mashabiki hao waliipata baada ya kiungo wao, Gerson Fraga raia wa Brazil kufunga mabao mawili na kuwapa pointi tatu  Simba mbele ya Coastal Union.

 

Kiungo huyo kwa mara ya kwanza aliibuka tena katika kikosi cha kwanza cha Simba baada ya kuzikosa mechi sita mfululizo na kuja kuibuka shujaa kwa kufunga mabao hayo katika ushindi walioupata wa mabao 2-0.

Fraga alifunga bao la kwanza kwa kichwa akiunganisha krosi ya Clatous Chama dakika ya saba kipindi cha kwanza. Mbrazili huyo aliihakikishia Simba pointi tatu baada ya kuweka bao la pili akimalizia kirahisi mpira uliopigwa na Hassan Dilunga dakika ya 78 na kuifanya Simba kuibuka kifua mbele.

 

Kwa sasa Simba wanazidi kukaa kileleni wakiwa na pointi 47 baada ya kucheza mechi 18 na kushinda mechi 15, huku wakiiacha Yanga pointi 19 ikiwa imecheza mechi 15. Leo Jumapili Yanga ambao Mghana wao, Bernard Morrison akiwa uwanjani ana mbwembwe za kutembea juu ya mpira, itacheza dhidi ya Mtibwa Sugar uwanjani hapo.

Leave A Reply