The House of Favourite Newspapers

Okwi Afungukia Dili La Kutua Sauz

 

EMMANUEL Okwi anaamini kwamba kama dili yake na Kaizer Chief ya Afrika Kusini ni ya kweli ataruhusiwa baada ya mechi ya Jumapili dhidi ya Nkana Jijini Dar es Salaam.

 

Katika mechi hiyo ya marudiano ya raundi ya kwanza ya Ligi ya Mabingwa Simba inahitaji ushindi wa bao 1-0 tu kufuzu makundi baada ya kufungwa mabao 2-1 kwenye mechi ya awali.

 

Akizungumza na Championi Jumatano, Okwi alisema; “Ni kweli nimesoma tetesi za mimi kuhitajika katika timu ya Kaizer Chiefs ya Sauz, ila sijapata taarifa hizo rasmi kutoka kwa uongozi wangu wa Simba nadhani wanashindwa kuniambia kutokana na ugumu wa michuano tunayoshiriki.”

 

“Naamini kila mmoja wetu yuko makini na michuano hii hivyo nafikiri kama mpango huo upo wataniambia baada ya kumaliza kwa mchezo wetu ujao dhidi ya Nkana ya Zambia Desemba 23 hapa nyumbani.

 

“Natambua kila mtu angependa sana kujua juu ya suala hili lakini ukweli ni kwamba mara tu nitakapojuzwa juu ya ofa hiyo sitasita kuwaeleza mashabiki zangu kupitia vyombo vya habari kwani kama ishu ipo wazi mimi sioni haja ya kuendelea kukaa kimya. Ingawa, kwa kipindi hiki kwetu ni kigumu kwani mawazo na masikio yetu sasa yanatazamia ushindi katika mchezo ujao tu,” alisema Okwi.

 

Comments are closed.