The House of Favourite Newspapers

Okwi azua balaa Simba, aondolewa kikosini

Mganda, Emmanuel Okwi.

KIKOSI cha Simba, leo jioni kinatarajiwa kutua mjini Shinyanga kwa ajili ya mechi ya Ligi Kuu Bara dhidi ya Stand United itakayochezwa kwenye Uwanja wa Kambarage mjini humo keshokutwa Jumapili.

 

Hata hivyo, mshambuliaji wa kutumainiwa wa timu hiyo, Mganda, Emmanuel Okwi ataukosa mchezo huo ambao unatarajiwa kuwa na ushindani mkubwa jambo ambalo limezua hofu kubwa kwa mashabiki wa timu hiyo.

 

Mmoja wa viongozi wa benchi la ufundi la Simba ambaye ameomba kutotajwa jina lake, ameliambia Championi Ijumaa kuwa, Okwi atau­kosa mchezo huo ili aweze kupona vizuri jeraha lake aliloumia chini ya jicho katika mchezo wa ligi kuu dhidi ya Azam FC.

 

Okwi alipata jeraha hilo baada ya kugongana na kiungo msham­buliaji wa Azam FC, Mghana Enock Agyei wakati waki­wania mpira na kujikuta akidondoka chini na kupoteza fahamu.

 

“Kwa hiyo, katika mechi yetu hiyo na Stand, Okwi hatakuwepo na hivi sasa yupo Dar es Salaam, kocha alimruhusu aje kupumzika kwani katika mechi dhidi ya Lipuli alicheza lakini alikuwa akilalamika kuwa na maumivu makali.

 

“Jambo hilo limemfanya kocha achukue uamuzi huo wa kumrudi­sha Dar ili apate muda wa kutosha wa kupumzika lakini pia matibabu ya jeraha hilo ili aweze kupona kabla ya safari yetu ya Algeria kwa ajili ya mchezo wetu wa marudiano na JS Saoura,” kilisema chanzo hicho cha habari.

 

Hata hivyo, Meneja wa Simba, Patrick Rweyemamu alipoulizwa kuhusiana na hilo alisema: “Ni kweli Okwi ataukosa mchezo wetu dhidi ya Stand baada ya kuamua kumpumzi­sha kutokana na jeraha alilopata tulipocheza na Azam FC, pia katika msafara wetu wa Shinyanga hayupo.”

Comments are closed.